TENDENI HAKI KWA WATU WOTE BILA KUPOKEA WALA KUTOA RUSHWA-PROF. OLE GABRIEL

Na. Omary Mtamike, DODOMA

Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel ametoa wito kwa watendaji na watumishi wa Sekta hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano na kutenda haki wakati wote wanapotoa huduma kwa wananchi.

Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza kuhusu dhana ya “uwajibikaji wa watumishi kwa haki” mbele ya watumishi na watendaji wa Wizara hiyo wakati wa hafla fupi ya kumuaga iliyofanyika leo (30.08.2021) kwenye viwanja vya Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Magufuli eneo la Mtumba jijini Dodoma


Prof. Ole Gabriel ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama nchini kwa hivi sasa ameyasema hayo leo (30.08.2021) katika halfa fupi ya kumuaga iliyofanyika kwenye viwanja vya Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Magufuli eneo la Mtumba jijini Dodoma. “Ni vizuri muendelee kutambua kuwa nyie ni watumishi wa umma na kazi yenu kubwa ni kutatua changamoto za watanzania kupitia sekta ya Mifugo hivyo mfanye hivyo kwa kutenda haki bila gharama bila rushwa”.

Aidha Prof. Ole Gabriel amemshukuru Rais mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho kikwete na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwa wa kwanza kutambua uwezo wake na kumteua kutumikia kwenye nafasi ya katibu Mkuu katika Wizara mbalimbali. “Ninatambua kazi niliyonayo hivi sasa ni kubwa sana lakini ninamuahidi Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa nitaitumikia nafasi aliyoniamini kwa mafanikio makubwa na kuleta mabadiliko anayoyatarajia katika eneo hili la Mahakama” Amesema Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel alihitimisha hotuba yake kwa kutoa rai kwa watumishi hao wote kujali afya zao wakati wote ikiwa ni pamoja na kuchukua tahadhari ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Uviko 19. Akizungumza kwa niaba ya wafugaji wote nchini, Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji (CCWT), Jeremiah amesema kuwa Prof. Ole Gabriel amefanikiwa kuwapa muongozo wa namna bora ya kukiendesha chama chao ili kiweze kuwapa manufaa wafugaji tofauti na hapo awali ambapo chama hicho kilikuwa kikijiendesha kama chama cha wanaharakati.

Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel akionesha zawadi aliyopewa na watendaji na watumishi wa Wizara hiyo wakati wa hafla fupi ya kumuaga iliyofanyika leo (30.08.2021) kwenye viwanja vya Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Magufuli eneo la Mtumba jijini Dodoma


“Ni kwa jitihada zako hizi ndio maana leo tumefanikiwa kutatua changamoto nyingi zilizokuwa zikiwakabili wafugaji na kwa heshima kubwa ninaomba nikukabidhi ng’ombe mmoja kama zawadi kutoka kwenye chama chetu” Amesema Jeremiah.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi wote wa Sekta ya Mifugo, Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Mifugo, Prof. Hezron Nonga amemshukuru Prof. Ole Gabriel kwa kutenda haki na kujali usawa kwa watumishi wakati wote wa utekelezaji wa majukumu yao. “Kwa kweli umekuwa ukipambana usiku na mchana na kutukumbusha mara nyingi kuhusu kuwajali watumishi wa kada nyingine wanaotusaidia kwenye kazi mbalimbali ofisini na kwa ujumla wake hukupenda kuona mtumishi yoyote anaonewa” Amesema Prof. Nonga.

Prof. Nonga amebainisha kuwa watumishi wote wa Sekta ya Mifugo wataendelea kuenzi utaratibu wa kutunza thamani ya muda jambo ambalo lilisisitizwa mara zote na Prof. Ole Gabriel wakati wakati wa uongozi wake. “Lakini pia wakati wote ulisisitiza kufanya kazi kimkakati ikiwa ni pamoja na “kubrand” Wizara kupitia njia mbalimbali na kudumisha ushirikiano baina yetu na Taasisi mbalimbali” Amesema Prof. Nonga. 

Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel (wa tatu kutoka kulia mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi,watendaji na watumishi mbalimbali wa Wizara hiyo wakati wa hafla fupi ya kumuaga iliyofanyika leo (30.08.2021) kwenye viwanja vya Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Magufuli eneo la Mtumba jijini Dodoma


Prof. Elisante Ole Gabriel ametumikia nafasi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) kwa kipindi cha miaka mitatu na moja ya kazi kubwa aliyoifanya wakati akitumikia nafasi hiyo ni kuboresha mazingira ya uwekezaji kwenye sekta hiyo.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.