PROFESA MKENDA AELEZA SABABU YA KUTOTOA KIBALI CHA UAGIZAJI WA SUKARI NCHINI

 


Na Rhoda Simba, Dodoma.

ILI kuvisaidia viwanda  vya ndani viweze kuzalisha sukari kwa wingi Waziri  wa Kilimo,Profesa Adolf Mkenda amesema katu hatotoa kibali cha uagizaji  wa sukari nchini kwa mtu yeyote.  

Akiongea leo Agosti 30,2021,wakati wa uzinduzi wa matokeo ya sensa ya kilimo, mifugo na uvuvi ya mwaka 2019-2020 ulioandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS),Waziri Mkenda amesema suala la uingizaji wa sukari nchini limejaa rushwa ambapo amedai ni kama madawa ya kulevya kwani imekuwa ikiwanufaisha watu wachache.

Amesema huku nyuma kuna baadhi ya Mawaziri waliondolewa sababu ya sakata la utoaji wa vibali vya uingizaji wa sukari ambapo amedai Serikali ya awamu ya tano na sita imejipanga kuhakikisha inavisaidia viwanda vya ndani.

Waziri Mkenda amesema kwa sasa mwenye Mamlaka ya kutoa kibali cha uingizaji wa sukari ni Waziri wa Kilimo ambaye ni yeye hivyo hatotoa kwa mtu yeyote lengo likiwa ni kuvisaidia viwanda vya ndani.

“Bunge ndio limepitisha kibali cha ukitaka kuagiza sukari lazima uwe ni mzalishaji wa sukari na mwenye uwezo wa kuzlaisha tani 40,000 na hakuna ambaye ataagiza sukari mpaka kuwe na pengo,kibali kitapita kwangu na hakitapita bora niachie ngazi tunamnufaisha nani,wanaopeleka majungu wapeleke tu juzi nimefuatwa Uwanja wa ndege,hatutoi kibali NG’O,”amesema.

Hata hivyo amesema iwapo sheria ya uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi itabadilishwa atakuwa tayari kujiuzulu kwani itakuwa imewabeba watu wenye fedha.

Kuhusiana na bei ya mafuta kuwa juu,Waziri Mkenda amesema Wizara imeweka mikakati ya kuhakikisha mbegu ya zao la Alizeti inapatikana kwa wingi.

Vilevile, amesema Serikali imejipanga kuweka mikakati ya pamoja kuhakikisha mbolea inapatikana kwa wingi.

Kuhusiana na uzinduzi matokeo ya sensa ya kilimo, mifugo na uvuvi ya mwaka 2019-2020, Waziri Mkenda amesema sensa hiyo imewasaidia kufanya uchambuzi namna ya kufanya kilimo na ufugaji bora ambapo amedai sekta ya mazao inachangia asilimia 15 ya pato la Taifa.

Amesema wanaojishughulisha na mazao ni  ni asilimia 60 lakini katika pato la Taifa wanachangia kwa asilimia 15 ambapo amedai haki hiyo inaonesha kwamba watanzania wanaumaskini mkubwa hasa wa maeneo ya vijijini,uwiano wa sekta za uchumi ni mbaya pamoja na tija ndogo katika sekta ya kilimo.

Kwa upande wake, Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dkt.Albina Chuwa amesema lengo la sensa hiyo ni kutoa taarifa  katika uzalishaji wa mazao,idadi ya mifugo na ufugaji wa samaki  ambapo amedai wametumia mfumo wa kidigitali kukusanya takwimu mbalimbali.

Amesema wametumia shilingi bilioni 6 ukilinganisha na mwaka 2007-8 ambapo walitumia shilingi bilioni 10 ambapo walitumia fedha nyingi katika makaratasi.

Dkt Chuwa amesema wametumia mwezi mmoja kutangaza matokeo ya utafiti tofauti na miaka ya nyuma ambapo walikuwa wakitumia miaka miwili  hadi mitatu.

Naye,Mkuu wa Wilaya ya Dodoma,Jabir Shekimweri ameiomba Wizara ya Kilimo kufungua duka la mbegu ambalo litawasaidia wakulima kuweza kununua mbegu bora kwani wengi wamekuwa wakiuziwa mbegu feki.

Mwisho

 

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.