MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA AMTAJA DKT. KIKWETE KWA KUMJENGEA MSINGI

             Na. Edward Kondela

 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema anamshukuru sana Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuwa ndiye aliyemuibua katika uongozi mwaka 2013 kwa kumteua kwa mara ya kwanza kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana, Utamadani na Michezo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto), akimkabidhi nyaraka muhimu za ofisi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayoshughulikia Mifugo Bw. Amosy Zephania ambaye ana kaimu nafasi hiyo kwa sasa, mara baada ya Prof. Gabriel aliyekuwa akihudumu nafasi hiyo kuteuliwa hivi karibuni na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania


 

Prof. Gabriel amebainisha hayo (30.08.2021) wakati akizungumza na menejimeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika ofisi za wizara hiyo jijini Dodoma, wakati alipofika kwa ajili ya kukabidhi ofisi aliyokuwa akihudumu katika nafasi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo.

 

Aidha, Prof. Gabriel amebainisha kuwa siku chache kabla ya Mhe. Dkt. Kikwete kuondoka madarakani Mwezi Oktoba Mwaka 2015, alimteua kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana, Utamadani na Michezo hivyo hana budi kumshukuru kwa kuwa alionesha imani kubwa kwake.

 

Pia, amesema anashukuru aliendelea kuaminiwa na Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ambaye alimteua kushika nafasi ya Katibu Mkuu wizara tofauti na Rais wa Awamu ya Sita Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye alimteua kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo nafasi ambayo alikuwa akiendelea kuihudumu hadi alipomteua tena hivi karibuni kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza na menejimenti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi sekta ya mifugo pamoja na baadhi ya viongozi wa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, wakati alipowasili katika ofisi za wizara hiyo zilizopo jijini Dodoma kwa ajili ya kukabidhi ofisi aliyokuwa akihudumu kwenye nafasi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo kabla ya kuteuliwa hivi karibuni na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania


 

“Namshukuru sana Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwa na imani nami katika nafasi hii mpya aliyoniteua ya kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, na kwamba nitafanya kazi kwa nguvu na weledi mkubwa kwa kushirikiana na wenzangu kwa kuwa nina deni kubwa la kulipa kwa Mhe. Rais Samia, lakini pia kufikia matarajio ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Juma na matarajio ya watanzania wote katika mhimili huu kwenye utendaji wa haki.” Amesema Prof. Gabriel

 

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amefanya mazungumzo na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (Mb), katika ofisi za wizara hiyo ambapo Waziri Ndaki amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa na imani kubwa na Prof. Gabriel kwa kumteua kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kutoka katika nafasi aliyokuwa akihudumu ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo.

 

Waziri Ndaki amesema uteuzi aliopata, Prof. Gabriel kusimamia mhimili muhimu katika taifa hili kwenye masuala yanayohusu haki kwa watanzania na kwamba jambo hilo ni kubwa kwa kuwa ni mhimili muhimu kwa taifa.

 

“Mimi nikupongeze kwa kuaminiwa kwa kiasi hicho, kwa sababu ni kwa kiasi kikubwa kwa kweli lakini nichukue nafasi hii kukushukuru kwa muda ambao tumefanya kazi pamoja.” Amesema Mhe. Ndaki.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel, akiangalia zawadi ya kadi maalum iliyoandaliwa kwa ajili yake kutoka kwa menejimenti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi sekta ya mifugo, katika ofisi za wizara hiyo zilizopo jijini Dodoma, mara baada ya kukabidhi ofisi aliyokuwa akihudumu katika nafasi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo kabla ya kuteuliwa hivi karibuni na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania


 

Mhe. Ndaki amesema wakati Prof. Gabriel alipokuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika sekta ya mifugo amekuwa msaada mkubwa kwake katika utendaji kazi na kwamba amekuwa akitoa maelekezo na usimamizi wa majukumu mbalimbali ya wizara na kutengeneza timu ambayo inaelewa majukumu yake.

 

Ameongeza kuwa wakati wa uwepo wake katika wizara hiyo Prof. Gabriel amekuwa ni mtu wa kujitolea na kufanya kazi muda wowote bila kujali siku wala saa na kwamba watumishi wengi wa wizara wanaweza kufanya mambo makubwa na wizara itaendelea kuhitaji ushirikiano wake wa karibu kwa ajili ya kupata uzoefu kutoka kwake kwa yale aliyokuwa akisimamia wizarani hapo.

 

Awali mara baada ya kukabidhiwa nyaraka muhimu za ofisi ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayoshughulika na Mifugo, Kaimu Katibu Mkuu Bw. Amosy Zephania amemshukuru Prof. Elisante Ole Gabriel wakati wa utumishi wake wa miaka mitatu katika wizara hiyo kwa kuwa amejenga msingi mkubwa wizarani hapo.

 

Picha ya pamoja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (Mb), (katikati), Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (Kushoto) ambapo hapo awali alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo pamoja na Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo sekta ya mifugo Bw. Amosy Zephania, mara baada ya Prof. Gabriel kufika katika ofisi za wizara hiyo zilizopo jijini Dodoma kukabidhi ofisi aliyokuwa akihudumu kama Katibu Mkuu sekta ya mifugo ambapo hivi karibuni ameteuliwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania


Bw. Zephania amefafanua kuwa atahakikisha anasimamia misingi iliyoachwa na Prof. Gabriel na kuhakikisha anaisimamia vyema sekta ya mifugo ili iendelee kuleta tija kwa wananchi hususan wafugaji na kuzingatia yote ambayo mtendaji mkuu huyo wa mahakama amewaachia yakiwemo ya kushirikiana kwa viongozi na wafanyakazi wote kwa ujumla.

 

Mwisho.

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.