TUMIENI VYAMA VYA USHIRIKA KUTAFUTA SOKO LA MAHINDI -RC MKIRIKITI

Na. Revocatus Kassimba, SUMBAWANGA

Wanachi wa kijiji cha Ntendo Manispaa ya Sumbawanga wameiomba serikali kusaidia kupatikana kwa soko la mazao yao ikiwemo mahindi ili waweze kupata fedha za kuchangia shughuli za maendeleo ikiwemo ujenzi wa zahanati na madarasa ya shule.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga Jacob Mtalitinya (kulia) akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa shule mpya ya msingi Ntendo B kwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Joseph Mkirikiti (kushoto aliyevaa suti nyeusi) leo wakati wa ziara ya Mkuu huyo wa Mkoa kukagua miradi ya maendeleo


Wametoa maombi hayo kwa nyakati tofauti wakati wakiongea na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti alipotembelea kijiji hicho kukagua mradi wa ujenzi wa shule mpya ya msingi ya Ntendo B ambapo ilianza kujengwa mwaka 2018.

“Kero tuliyonayo hapa Ntendo ni soko la mazao sasa mahindi tunauza kwa bei ya chini  ambapo sado moja  inauzwa shilingi 800. Mimi mwaka huu nimepata gunia 40 na sasa nimeshindwa kuuza, yapo tu nyumbani. Serikali itusaidie” alisema mkazi wa Ntendo James Zumba kwenye mkutano huo.

Eliza Kachele alisema kero nyingine ya kijiji cha Ntendo ni mrundikanao wa wanafunzi kwenye shule ya msingi ambapo inasababisha wanafunzi kutosoma vizuri hivyo ameitaka Serikali kutoa fedha kukamilisha shule mpya ya msingi ya Ntendo B inayojengwa.

Akijibu hoja za wananchi wa kijiji cha Ntendo, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti aliwashukuru wananchi hao kwa kujitokeza kwenye mkutano huo na kuwasilisha kero zao.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Joseph Joseph Mkirikiti akiongea na wafanyabiashara wa soko dogo la kijiji cha Ntendo Manispaa ya Sumbawanga ambapo ameagiza wawekewe mazingira mazuri ikiwemo paa na vibanda kujikinga na jua pia mvua


Mkirikiti aliwaeleza wanachi hao kuwa Serikali inaendelea kutafuta ufumbuzi wa soko la mahindi ambapo amewaeleza kuwa mahindi bado yanahitajika nje ya nchi hivyo endapo mfumo wa ushirika ukitumika unaweza kusaidia upatikanji soko.

“Mzizi pekee wa kufanya mahindi yapate bei ni kuacha kuuza kiholela . Ili tuuze mahindi vizuri tuna jukumu la kuimarisha vyama vya ushirika viweze kutafuta soko la uhakika la mahindi ili mkulima apate fursa ya soko. Mfumo wa kila mtu kutafuta soko la mahindi unasababisha wakulima wanyonywe” alisema Mkirikiti.

Mkuu huyo wa Mkoa amewasihi wananchi kufuata ushauri uliotolewa na Serikali endapo wanapata soko la mahindi nje ya nchi wasiwekewe vikwazo bali wasaidiwe kulifikia soko hilo.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa ameagiza Manispaa ya Sumbawanga kuboresha mazingira ya soko la wananchi wa Ntendo kwa kuliwekea miundombinu ikiwemo paa na vibanda ili waepukane na jua na mvua ambayo ni kero kwa sasa.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Joseph Mkirikiti (katikati) akiwa kwenye ukaguzi wa jengo la maabara ya baiolojia katika shule ya sekondari Kalangasa Manispaa ya Sumbawanga leo ambapo ameitaka Manispaa hiyo kukamilisha maabara zingine ili wanafunzi waweze kujifunza kwa vitendo masomo ya sayansi


Kuhusu ujenzi wa madarasa ya shule mpya ya Ntendo B Mkuu huyo wa Mkoa wa Rukwa ameagiza Manispaa ya Sumbawanga kukamilisha ujenzi wake kabla ya mwezi Oktoba mwaka huu ili kuwa na uhakika wa kupunguza msongamano kwenye shule iliyopo .

Akizungumzia mkakati wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, Jacob Mtalitinya alisema katika mwaka huu fedha 2021/22 wamepanga kukamilisha jumla ya vyumba 72 vya madarasa kwa kutumia fedha za mapato ya ndani ya ili kuwa na uhakika wa mapokezi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2022.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Rukwa anaendelea na ziara ya kikazi Manispaa ya Sumbawanga kuzungumza na wananchi na kukagua miradi ya maendeleo.

 

Mwisho

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.