BARAZA LA WAZEE MKOA WA DODOMA LAZINDULIWA

Na. Noelina Kimolo, DODOMA

 

SERIKALI mkoani Dodoma imewahakikishia wazee kuwa itaendelea kusimamia sera ya wazee kwa lengo la kuwahakikishia upatikanaji wa huduma bora kwa ustawi wa maisha yao kutokana na mchango wao mkubwa katika uchumi wa Tanzania.

Khamis Mkanachi akiongea na Baraza la Wazee Mkoa wa Dodoma


Hakikisho hilo lilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kondoa, Khamis Mkanachi alipomuwakisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, katika hafla fupi ya uzinduzi wa Baraza la Wazee la Mkoa wa Dodoma lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Mkanachi alisema kuwa serikali kupitia Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 imeeleza kuwa wazee ni kundi muhimu katika jamii na wanapaswa kutambuliwa na kupewa fursa ya kushiriki katika mambo yanayohusu maisha ya kila siku kwa manufaa ya watanzania wote. Vilevile, inahakikisha wazee wanapata huduma zote muhimu ambazo zitawawezesha kushiriki kwa ukamilifu katika Maisha kila siku. Hivyo, ustawi wa wazee ni wajibu wa serikali, aliongeza.

“Serikali inaendelea kuwahudumia wazee katika upande wa afya, lishe na huduma zote za msingi ili kukidhi mahitaji ya mwanadamu huu ni wajibu wa msingi ambao serikali yetu imeuchukua” alisema Mkanachi.



Akiongelea uongozi wa baraza la wazee uliochaguliwa, alisema kuwa unawajibu wa kuwasaidia na kuwatetea wazee ili waweze kusimamia haki na ustawi katika kupewa kipaumbele kwenye huduma mbalimbali.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma, Nathalis Linuma alisema kuwa anatambua msaada utolewao na wazee kwa kuwa hata viongozi wengi kabla ya kufanya maamuzi huwa wanawashirikisha wazee katika maamuzi yao.

“Na utamaduni huo umekuwa ukiendelea kila siku na ndio maana hata sisi tukaona ni muhimu kuwa na Baraza la Wazee katika kuleta maendeleo ya taifa’’ alisema Linuma.

Nae Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Mkoa wa Dodoma, Mchungaji Petro Mpolo alisema kuwa ni muhimu kwa wazee kujua haki zao katika kufanya maamuzi ili kuleta maendeleo katika jamii.

“Sisi wazee tunayo mambo mengi ambayo serikali tunahitaji mtusaidie. Wazee waliochaguliwa kuanzia ngazi ya Kata hadi Mkoa hawajui kazi yao na mipaka hivyo, tumeomba kupewa semina za mabaraza ya wazee ili watambue wajibu wao katika kazi zao” alisema Mchungaji Mpolo.

Pia ameomba halmashauli ziwe zinatenga bajeti za kuwawezesha wazee kutekeleza majukumu yao kuanzia ngazi za chini hadi juu.

 


MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.