Na. Catherine Sungura, WAMJW-Kilimanjaro
Waziri wa
Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima, jana ametembelea uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ikiwa ni
kufuatilia utekelezaji wa muongozo namba 7 wa ushauri wa wasafiri wanaoingia
nchini uliotolewa tarehe 4 Mei, 2021.
Katika
muongozo huo moja ya maelekezo ni kufanya uchunguzi wa COVID-19 kwa kuwapima
kipimo cha haraka (Rapid Test) wasafiri wote wanaoingia nchini, kwani kumekuwa
na malalamiko kadhaa kutoka kwa wananchi kuhusu zoezi hilo. Mojawapo ya malalamiko
hayo ni abiria kuchelewa kumaliza hatua za huduma ya vipimo vya afya.
Mhe.
Waziri amebaini kuwa watumishi wapo na wanafanya kazi zao vizuri wakiwemo
maafisa afya, maabara na watumishi wa uwanja wa ndege. Waziri amewapongeza
watumishi hao kwa kazi nzuri wanaoifanya. Aidha, amewashukuru viongozi wa mkoa
wa Kilimanjarao na Halmashauri ya Hai, Moshi kwa kutoa watumishi wa ziada ili
kuongeza nguvu.
Amesema
kuwa abiria kuchelewa kumaliza hatua za vipimo vya afya pia inachangiwa na
baadhi yao kutojaza taarifa zao za hali yao ya afya kupitia mfumo wa
kieletroniki wa afyamsafiri ambao unamtaka abiria kujaza taarifa zake ndani ya
masaa 24 kabla ya kuingia nchini na hivyo kuwafanya wachelewe kuanza hatua ya
uchunguzi wa awali (primary screening) na mwisho kufanya hatua zote za kulipia
na kupima kuchelewa pia.
Aidha,
ametoa wito kwa mashirika ya ndege na mamlaka ya viwanja vya ndege, usafiri wa
ndege na wakala wa ndege, mabasi kushirikiana kutoa elimu ili taarifa hizo
zijazwe mapema kabla ya kufika katika maeneo yetu ya viwanja vya ndege, bandari
na mipaka yote.
Kwa upande
wa vipimo vya awali ameelekeza ufanyike utaratibu wa kuongeza idadi ya wapimaji
kutoka watano hadi kufikia 8 na wakati huo uratibu ufanyike kuomba wahasibu
kutoka wizara ya fedha kwa ajili ya kuratibu malipo kwa ushirikiano na banki
husika na wataalamu wa afya wahusike na kuongeza nguvu ya kutoa huduma za afya.
Pia kwa
kuzingatia kuelekea msimu wa wageni wengi wizara itashirikiana na wadau wake
kuimarisha huduma za vipimo vya haraka huku ikiendelea kupokea maoni mbalimbali
na kuyafanyia kazi. Vilevile, amesema wizara itaendelea kuboresha mfumo wa
afyamsafiri ili uweze kurahisisha taratibu za kuwahudumia wasafiri kabla
hawajaanza safari na kupunguza changamoto mbalimbali wanazolalamikia wakati
wanapowasili nchini.
Comments
Post a Comment