MKURUGENZI AWAHIMIZA WATALAAMU WA MAJENGO KUWEKA MIUNDOMBINU RAFIKI KWA WATU WENYE ULEMAVU

 

Watumishi wa vituo vya afya na zahanati kutoka kata 5 za wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Kongwa Dk Omary Nkullo (hayopo pichani) alipokuwa akifungua mafunzo ya afya yaliyoandaliwa na Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) yaliyofanyika Kongwa 

Na Mwandishi Wetu,Kongwa.

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Kongwa Dk Omary Nkullo, amewataka wataalamu wa majengo kuhakikisha wanawaeka miundombinu rafiki itakayo wawezesha watu wenye ulemavu kupata huduma stahili kama ilivyo kwa wengine wasio na ulemavu.

Dk Nkullo amesema hayo alipokuwa akifungua mafunzo ya siku moja kwa watumishi wa vituo vya afya na zahanati kutoka kata 5 za wilaya hiyo juu ya upatikanaji wa huduma jumuishi za afya kwa watu wenye ulemavu iliyofanyika Kongwa.

Alisema kuwa majengo mengi yaliyojengwa miaka ya nyuma wilayani humo hayana miundombinu rafiki kwa wenye ulemavu suala ambalo linaloonyesha bado kuna unyanyapaa na ubaguzi kwa upande wao.

“Hata hapa ofisini kwangu jengo hili naona lilisaulika wataalam hawakuweka miundombinu rafiki ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kuingia kwa urahisi hapa,cha kusikitisha hata huko kwenye vyoo havipo vinavyoweza kutumia na ndugu zetu hao huu ni unyanyapaa na tena ni ubaguzi”alisema.

Hata hivyo amewataka wahudumu wa afya kuonyesha upendo kwa vitendo kwa watu wenye ulemavu  wanapo wahudumia kulingana na aina ya ulemavu badala ya kuwanyanyapaa na kuwabagua.

Kwa upande wake Katibu wa Mkoa wa wa Dodoma Shirikisho la watu wenye ulemavu (SHIVYAWATA) Justust Ng’wantalima alisema kuwa unyanyapaa na ubaguzi bado unawakatisha tamaa pindi wanapougua na kushindwa kupata huduma ya kiafya.

“Pamoja na sababu zingine za kiuchumi,kitaasisi na kijamii zinazowakabila watu wenye ulemavu,unawakatisha tamaa na kufikia hatua ya kuficha hali zao pale wanapougua na kufikia hatua ya kuacha kutafuta matibabu”alisema”alisema.

Naye Mtabibu wa afya Zahanati ya Mautya Kongwa Suzana Petro,ameiomba serikali kutoa elimu ya kutosha kwa wahudumu wa afya na zahanati vilivyopo vijijini ili waweze kuwahudumia ipasavyo kulingana na ulemavu alionao.

Mwisho.

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.