BIMA ITAWAKOMBOA WAFUGAJI NA WAVUVI NCHINI-ULEGA

Na. Omary Mtamike, DODOMA

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah ulega ameliagiza Dawati la Sekta binafsi lililopo Wizarani hapo kushughulikia  haraka mchakato wa upatikanaji wa huduma ya bima kwa wafugaji na wavuvi ili waweze kutekeleza kwa tija shughuli zao.

Ulega ameyasema hayo wikiendi hii wakati akipokea taarifa ya mafanikio ya Dawati hilo tangu kuundwa kwake ambapo alibainisha kuwa wapo wanunuzi wakubwa wa mazao ya mifugo na uvuvi ambao huwa hawalipi papo kwa hapo jambo ambalo mara nyingi huwafanya wafugaji na wavuvi kushindwa kufanya biashara kutokana na ukosefu wa mtaji.

“Msimu wa sikukuu ya Eid ya kuchinja (Eid-El-Haji) mimi ninamfahamu mtu mmoja kutoka uarabuni ambaye huwa anachinja hadi ng’ombe 15,000 na  huwa ananunua kwa wafugaji wetu hapa nchini lakini changamoto kubwa ni kwamba wafanyabiashara wengi hasa hawa wa kutoka nchi za kiarabu hawalipi papo kwa hapo hivyo kwa wafanyabiashara wetu wa ndani inakuwa ngumu kufanya nao biashara kwa sababu hawana mitaji mikubwa kiasi hicho na bahati mbaya hawakopesheki hivyo ni lazima mazungumzo na Shirika letu la Bima yafike mwisho ili hatimaye sasa  tuzialike taasisi za fedha ziweze kuwawezesha wafugaji na wavuvi wetu hapa nchini ” Aliongeza Ulega.

Kwa Upande mwingine Ulega ameiagiza Idara ya Uzalishaji na Masoko kwa kushirikiana na Dawati la sekta binafsi kuongeza wataalam wa utafiti na ubunifu wa masoko ili waweze  kurahisisha upatikanaji wa mahitaji ya soko, changamoto za huduma ambazo wadau wa sekta za mifugo na  uvuvi wanakumbana nazo, hali ya soko na mabadiliko ya huduma ambayo inahitajika sokoni.

“Hawa wataalam wanaweza kupata “link” na Ofisi nyingine za Serikali kama kituo cha uwekezaji na Wizara ya Viwanda na Biashara lengo likiwa ni kutujulisha na kutushauri kipi kinapungua na kipi kinazidi ili kila mara na kuangalia wadau wanasemaje kisha anatupa ushauri ili sisi kama viongozi tufanye maamuzi sahihi na kwa wakati sahihi” Alisisitiza Ulega.

Kwa upande wake Mtaalam wa benki kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB)  Zakayo Mphuru amesema kuwa kabla ya kuanzishwa kwa Dawati la Sekta binafsi mikopo kwa upande wa sekta za Mifugo na Uvuvi ilikuwa chini sana lakini hivi sasa mfumo wa uzalishaji wa sekta hizo unazivutia taasisi za fedha kuwekeza fedha zaidi.

“Benki ya kilimo bado tuna mikopo mingi na nimeshamkabidhi Msimamizi wa Dawati mikopo ambayo ipo kwenye ngazi ya mapitio hivyo tunaomba Wizara itusaidie ili kuboresha upande wa Utawala hasa usimamizi wa upande wa kutunza kumbukumbu za vyama ili benki iwe na uhakika kwamba hela inapotoka lazima irudi ili ikawasaidie na watanzania wengine” Alisema Mphuru.

Naye Afisa miradi mwandamizi kutoka Taasisi ya utafiti,ushauri na maendeleo (DALBERG) Jackson Mahenge amesema kuwa uwepo wa Dawati la sekta binafsi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi umerahisisha kwa kiwango kikubwa ufanyaji kazi wa Taasisi yao jambo ambalo limewapa shauku ya kutamani kuona Wizara nyingine zikiwa na Dawati hilo.

“Tumefanya kazi na Wizara tofauti lakini tumeanza kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Dawati la Sekta binafsi tangu mwaka 2018 na nikiri wazi kuwa tangu tuanze ushirikiano wetu tumepata fursa ya kufanya kazi na wadau tofauti  jambo ambalo linafanya tuanze kuona yale mabadiliko ambayo tumekusudia  katika sekta za Mifugo na Uvuvi “ Alihitimisha Mahenge.

Tangu kuanzishwa kwa Dawati la Sekta binafsi ndani ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wafugaji na wavuvi wameweza kunufaika kupitia mikopo mbalimbali ya fedha na nyenzo zinazowasaidia kutekeleza majukumu yao kwa tija.

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.