Na. Veronica Simba – TSC
Mkurugenzi wa
Huduma za Sheria kutoka Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC), Wakili Richard
Odongo, amewaasa wajumbe wa Kamati za Wilaya zinazosimamia Ajira na Maadili ya
Walimu, kutenda haki wanaposhughulikia mashauri ya walimu, pasipo kujali
mazingira magumu ambayo wakati mwingine yanaweza kuwaathiri wao pia.
Wakili Odongo
ametoa wito huo leo Aprili 29, 2021 jijini Mwanza, wakati akiwasilisha mada
inayohusu Majukumu ya Mamlaka za Nidhamu na Rufaa kwa Walimu katika mafunzo ya
Wajumbe wa Kamati husika za Wilaya, Kanda ya Ziwa.
Akifafanua,
ameeleza kuwa sheria inawataka watendaji hao kusimamia haki hata pale
inapotokea wanaotuhumiwa ni ndugu au rafiki zao.
“Shughulikieni
mashauri ya walimu wanaotuhumiwa kwa kufuata haki. Kama haki inakutaka kupita
katikati ya Mlima, pita hapohapo pasipo kupindisha, hata kama itakugharimu wewe
mwenyewe,” alisisitiza.
Katika hatua
nyingine, Wakili Odongo amewasisitiza wajumbe hao kuhakikisha wanazingatia
Sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu Na. 25 ya mwaka 2015 pamoja na Kanuni za
Utumishi wa Umma za mwaka 2003 katika kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya
walimu.
Sambamba na
hilo, amesema Kamati husika zinapaswa kuzingatia Taratibu Bora za Uendeshaji wa
Mashauri ya Nidhamu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2007 pamoja na Kanuni za
Kudumu za Utumishi wa Umma za mwaka 2009.
Awali,
wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mwenyekiti wa TSC, Prof. Willy Komba na Katibu
wa Tume hiyo, Mwl. Paulina Nkwama, waliwasisitiza washiriki wa mafunzo hayo
kuhakikisha kwamba wanaendelea kujenga taswira njema ya TSC kwa walimu kwa
kutenda haki.
Mafunzo hayo
ya siku mbili yanalenga kuwajengea uwezo wajumbe wa kamati husika ili waweze
kutekeleza majukumu yao ya kuwahudumia walimu kwa weledi.
MWISHO
Comments
Post a Comment