Na. Mwandishi Wetu ARUSHA
Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na
Wizara ya Mifugo na Uvuvi pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama
limewakamata watuhumiwa watatu kwa tuhuma za wizi na utoroshaji wa mifugo
maeneo ya mipakani.
Kwa mujibu wa
taarifa iliyotolewa mwishoni mwa wiki na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha,
Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Polisi, Salum Hamduni amesema jeshi hilo
limewakamata watuhumiwa hao katika tarafa ya Loliondo, Wilaya ya Ngorongoro
mkoani humo kufuatia agizo alilolitoa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki Jumatano iliyopita la
kukamatwa kwa watuhumiwa 67 wa utoroshaji wa mifugo na mazao yake.
Kamanda Hamduni
amesema kukamatwa kwa watuhumiwa hao watatu kunatokana na baada ya Wizara ya
Mifugo na Uvuvi kutangaza operesheni ya kudhibiti wizi na utororshaji wa mifugo
maeneo ya mipakani ambapo zilipatikana taarifa za uwepo wa watu wanaojihusisha
na wizi na utoroshaji wa mifugo katika Wilaya ya Ngorongoro.
Ameongeza kuwa
upelelezi bado unaendelea kuhusiana na tukio hilo, mara utakapokamilika jalada
litapelekwa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria.
Ametoa wito kwa
wananchi kuepuka usumbufu kwa kuhakikisha wanafuata sheria za biashara ya
usafirishaji wa mifugo kwani wasipofanya hivyo watakamatwa na kuchukuliwa hatua
kali za kisheria.
Jumatano ya wiki
iliyopita Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akiwa katika ofisi za
wizara hiyo zilizopo katika mji wa serikali Mtumba jijini Dodoma wakati
akiwasilishiwa ripoti ya uchunguzi, kuhusu utoroshaji wa mifugo mipakani
aliliagiza Jeshi la Polisi nchini Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo kuwakamata
mara moja watuhumiwa 67 wa utoroshaji wa mifugo na mazao yake kwenda nchi za
jirani.
Katika ripoti ya
uchunguzi, kuhusu utoroshaji wa mifugo mipakani, iliyowasilishwa na Kamishna
Msaidizi wa Jeshi la Polisi Julius Mjengi kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki imeeleza kuwa kabla ya
tarehe 7 Novemba, 2020, mifugo iliyokuwa inatoka kwenye minada ya awali ya
Handeni na Kilindi kuelekea nchini Kenya kupitia mpaka wa Horohoro haikuwa
inafuata taratibu za forodha kama shehena nyingine.
Aliongeza kuwa
takwimu za daftari la mifugo katika mpaka wa Horohoro zinaonyesha idadi ya
mifugo iliyopitishwa kuelekea nchini Kenya kwa kipindi cha miaka 17 kutoka
mwaka 2003 hadi Novemba, 2020 ilikuwa ni ng’ombe 24,980 na Mbuzi na Kondoo
9,368 (sawa na wastani wa Ng’ombe 122 na Mbuzi/Kondoo 46 kwa mwezi).
Taarifa hiyo
ilibainisha pia baada ya uchunguzi, ilionekana kuwa kati ya tarehe 7 Novemba,
2020 hadi tarehe 9 Desemba, 2020 (kipindi cha mwezi mmoja tu) jumla ya Ng’ombe
1,096 na Mbuzi na Kondoo 1,044 walipitishwa katika kituo cha Forodha kuelekea
nchini Kenya, ambapo huo ni wastani wa idadi ya mifugo iliyopita mpakani ndani
ya mwezi mmoja ukilinganisha na siku za nyuma.
Taarifa imebaini
pia viashiria vya udanganyifu wa kurekodi idadi sahihi ya mifugo inayokaguliwa
kwenda Kenya hususan katika mpaka wa Hororohoro – Tanga.
MWISHO
Comments
Post a Comment