WAZIRI JAFO AWAPONGEZA KONDOA MJI KUSIMAMIA UJENZI WA MADARASA

Na. Sekela Mwasubila, KONDOA

Waziri wa OR-TAMISEMI Mhe. Seleman Jafo amewapongeza viongozi na watumishi wa Halmashauri ya Mji Kondoa kwa kusimamia vizuri miradi ya ujenzi wa madarasa na kuwataka kuongeza juhudi katika kufanya kazi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma.

Waziri Selemani Jafo


Ameyasema hayo wakati wa ziara yake ndani ya Halmashauri ya Mji Kondoa ya ukaguzi wa miradi na kuongea na watumishi akiongozana na wataalam kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.

“Kabla ya kuja hapa nilipita katika miradi nimekagua jengo jipya la Halmashauri jengo ni zuri hongereni linaendana na nyie ila lipo nyuma ya muda sijaridhika ikifika Februari 1 nataka Mkurugenzi na watumishi wako mhamie kule lakini miradi ya ujenzi wa madarasa ipo vizuri ila wakati mwingine mzingatie ushauri nilioutoa ili tuwe na majengo yatakayodumu kwa mufa mrefu,” amesema Mhe. Jafo

Aidha amewashauri kuongeza mapato kwa kubuni vyanzo vipya ambavyo havitawaumiza wananchi ili kupata fedha za kutosha kwa ajili ya kuiendesha Halmashauri na kuondokana na utegemezi wa serikali japokuwa wanafanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato.

“Watumishi wote fanyeni kazi kwa kujituma zaidi na mnapopewa kazi zifanyeni kwa wakati ila kubwa fanyeni kazi kwa kupendana kwani muda mwingi watumishi mnautumia mkiwa kazini katika baadhi ya maeneo watumishi wa idara moja hawaongei hii inapunguza pia utendajikazi kwani wanaopendana hufanyakazi vizuri,” amesisitiza Mhe. Jafo

Aidha amewataka Idara ya maendeleo ya Jamii kusimamia asilimia kumi za mapato na kuhakikisha zinawafikia walengwa kwani katika baadhi ya maeneo fedha hizo zimekuwa hazitolewi kutokana na wakurugenzi kuzuia fedha hizo kutoka na kuahidi kusimamia mapitio ya kanuni za mikopo hiyo ili sehemu ya marejesho zitumike kwaajili ya ufuatiliaji wa mikopo hiyo.

Hata hivyo amewaagiza Makatibu Tawala wa mikoa kufanya tathmini ya bei za dawa kwa mshitiri na bei ya soko ili dawa zipatikane vituoni na amemuagiza Mganga Mkuu kufunga mfumo wa kielektroniki katika vituo vya afya na zahanati ili kuzuia wizi wa dawa.

Akiongea awali Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Suleman Serea amemshukuru Mhe. Waziri kwa ziara yake ndani ya mkoa wa Dodoma kwa ajili ya ukaguzi wa miradi ambapo serikali imetoa fedha nyingi za utekelezaji wa miradi na kumuahidi kusimamia maagizo yote yaliyotolewa ili kuhakikisha huduma inatolewa kwa wananchi.

Akimkaribisha Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kondoa Mkurugenzi Msoleni Dakawa amesema katika mwaka wa fedha 2017/18 halmashauri ilikisia kukusanya shilingi milioni mia 800 lakini mpaka kufika mwisho wa mwaka wa fedha ilikusanya shilingi bilioni 1.2 sawa na 133% na mwaka 2018/19 ilikisia kukusanya shilingi bilioni 1.6 mara mbili zaidi ya mwaka ulioisha na hadi kufikia 30 Juni 2019 Halmashauri ilikusanya shilingi 1.4 sawa na 88% hata hivyo kutokana na changamoto mbalimbali katika mwaka wa fedha 2020/21 imekisia kukusanya shilingi bilioni 1.4 na inaendelea kubuni vyanzo vingine vya mapato ili kukusanya mapato mengi zaidi bila kumuathiri mwananchi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kondoa, Mhe. Mohamed Kiberenge amemshukuru Mhe. Waziri kwa kuwatembelea na kumuahidi kufanya kazi kwa kushirikiana na Mkurugenzi na watumishi wote ambao ana imani kubwa nao kutokana na utendaji wao mzuri kwa lengo la kuibadilisha Halmashauri ya Mji Kondoa.

Ziara ya Mhe. Jafo imefanyika ikiwa ni mwendelezo wake wa kutembelea Halmshauri na kukagua miradi ambapo alipata fursa ya kutembelea ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Mji Kondoa lililoghalimu zaidi ya shilingi bilioni 3, ujenzi wa madarasa shule ya Msingi Maji ya Shamba na Shule ya Sekondari Ula ikiwa ni kati ya shule 7 zilizopokea shilingi milioni 291 na kuongea na watumishi.

 

MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.