Na. Edward Kondela
Serikali imesema inatafuta namna ya kuwa na
kituo kimoja cha kulipia tozo zote za mazao ya mifugo na uvuvi pamoja na
kuondoa tozo ambazo zinakwamisha sekta hizo zisikue.
Akizungumza jana (30.12.2020) na baadhi ya
wavuvi katika Kata ya Nyamikoma, iliyopo Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu, wakati
wa ziara yake ya siku moja mkoani humo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba
Ndaki amesema wizara itaangalia tozo ambazo zitakuwa rafiki kwa wawekezaji,
wafanyabiashara pamoja na wafugaji na wavuvi wa hali ya chini ili kuhakikisha
sekta za mifugo na uvuvi zinachangia kwa sehemu kubwa pato la taifa.
“Tutaenda kuangalia ni tozo zipi na baadhi
tayari mmeshazitaja zikiwemo za kusafirisha mazao ya mifugo na uvuvi nje ya
nchi halafu tunatafuta namna ya kuwa na kituo kimoja cha kulipia hizi tozo
zote.” Amesema Mhe.
Ndaki
Waziri Ndaki ambaye amefuatana na Naibu Waziri
wa wizara hiyo Mhe. Pauline Gekul ameongeza kuwa uwepo wa tozo ambazo zitakuwa
rafiki katika kukuza sekta za mifugo na uvuvi kutasababisha watu wengi kuwekeza
katika sekta hizo na kuongeza pato la taifa kwa kuwa shughuli za kuchumi
zitaongezeka.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mifugo na
Uvuvi Mhe. Pauline Gekul ameendelea kusisitiza kuwa watu wanaondelea
kujihusisha na uvuvi haramu kuacha mara moja vitendo hivyo kwa kuwa wizara
haitafumbia macho ambao bado hawataki kuacha kuharibu mazao ya uvuvi kupitia
vitendo hivyo.
Amesema ni wakati sasa jamii kushirikiana na
serikali kuwabaini watu wanaojihusisha na uvuvi haramu kwa kuwa wanaishi katika
maeneo wanayofahamika ili serikali ichukue hatua na kwamba Wizara ya Mifugo na
Uvuvi itazidi kutoa elimu juu ya athari ya uvuvi haramu kwa jamii na taifa kwa
ujumla.
Siku moja kabla ya kuanza ziara ya kikazi
Mkoani Simiyu, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki wakati
akihitimisha ziara ya siku mbili Mkoani Mwanza amefika katika Kijiji cha
Kitongosima kilichopo Wilaya ya Magu mkoani humo na kuzungumza na jamii ya
wavuvi na kuwasisitiza waanze kufuga samaki kupitia njia za vizimba na mabwawa
ili kujiongezea kipato na kuongeza kuwa mahitaji ya soko la samaki kwa sasa ni
makubwa.
Mhe. Ndaki amemuagiza Katibu Mkuu Wizara ya
Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Dkt. Rashid Tamatamah kuhakikisha
anaanzisha utaratibu wa kuwepo kwa kizimba cha mafunzo kwa ajili ya kufugia
samaki na kuhakikisha wataalamu kutoka wizarani wanafika katika kijiji hicho
kuwafundisha wananchi namna ya kufuga na kulisha samaki ili jamii ya hapo iweze
kupata mapato kupitia mazao ya uvuvi.
Waziri Ndaki amebainisha hayo baada ya
kutembelea vizimba vya kufugia samaki katika kijiji hicho vinavyomilikiwa na
Shamba la Konga na kufurahishwa na namna mwekezaji anavyofuga samaki kwa wingi
kwa njia ya vizimba ndani ya Ziwa Victoria kwa kuwa ni sera ya serikali
kuhakikisha katika kipindi cha miaka mitano ajira zaidi ya elfu arobaini na
tano zinapatikana kupitia ufugaji wa samaki.
Katika kuhakikisha wananchi wa Kijiji cha
Kitongosima wananufaika kupitia ufugaji wa samaki Mkurugenzi Mtendaji wa
Halmashauri ya Wilaya ya Magu Bw. Lutengano Mwalwiba amewataka wanakijiji hao
kujiunga katika ushirika ili halmashauri hiyo iweze kuwakopesha fedha kwa ajili
ya shughuli za uvuvi huku Mwenyekiti wa Chama cha Wafuga Samaki Ziwa Victoria
Bw. Cyprian Matembo amemuomba Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki
kuangalia namna wizara inavyoweza kuwasaidia kupata vyakula vya samaki kwa bei
nafuu kwa kuwa kwa sasa vyakula vingi vimekuwa vikiagizwa kutoka nje ya nchi na
kuongeza gharama za uzalishaji.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki
leo (31.12.2020) anahitimisha ziara ya kikazi katika mikoa mitatu ya Kanda ya
Ziwa kwenye Mkoa wa Shinyanga, baada ya kufanya ziara kwenye mikoa ya Mwanza na
Simiyu, akiambatana na Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Pauline Gekul.
MWISHO.
Comments
Post a Comment