DODOMA.
MWENYEKITI wa
Halmashauri ya Baraza Kuu la Waislamau Tanzania (BAKWATA) wilaya ya
Dodoma Bashiru Husseni,amewataka wazazi na walezi wa dini ya kiislamu kuwa
mstari wa mbele kuhakikisha wanawajibika katika kutoa misaada mbalimbali kwa
walimu wanaofundisha elimu ya Akhera na dunia kwenye vituo vya madrassa ili
waweze kujikwamua kimaisha.
Ushauri huo ametolewa na Mwenyekiti huyo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma baada ya kubaini miongoni mwa walimu wa vituo vya madrassa,hali zao kiuchumi kuwa ni ngumu na wanatakiwa kusaidiwa kifedha na mali.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa miongoni mwa walimu hao hali zao siyo mzuri kiuchumi,hivyo wazazi na walezi wa dini ya kiislamu wanatakiwa kuwajibika kuhakikisha wanasaidia walimu hao kwa kuwapatia michango mbalimbali ikiwemo mali na fedha, ili kazi wanazozifanya za kuwaelimisha watoto waweze kuzifanya kwa amani,upendo na furaha.
Hata hivyo amewashauri pia mashehe na maimamu wa misikiti kuwahamasisha waumini wao kuwa na moyo wa kupenda kujitolewa kutoa misaada mbalimbali ili ziwasaidie walimu hao ambao wamekuwa na mzigo mkubwa wa kuelimisha watoto katika maadili ya Kimungu.
“Mimi kama Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bakwata Wilaya ya Dodoma,ninawaomba ndugu zangu wa dini ya kiislamu na hata wale ambao siyo waislamu,toeni misaada yenu mbalimbali ili iwasaidie hao walimu wetu wa vituo vya madrassa ambao miongoni mwao wana kila sababu ya kusaidiwa kimaisha”alisema.
Hata hivyo amewataka Mashehe ndani ya misikiti kutumia nafasi zao kuwahamasisha wazazi na walezi wenye watoto wanaosoma na wale waliofaulu kwa mwaka huu kila mmoja kusiwepo na sababu ya kukaa majumbani.
“Kila mzazi na mlezi hakikishe mtoto wake anampeleka shule kupata haki yake ya kimsingi,ukizingatia kuwa serikali yetu tukufu imetupunguzia mzingo wa kusomesha,hivyo tutumie fursa hiyo ya kusaidiwa na serikali watoto wetu waende shuleni”
Hivyo Mashehe pamoja na viongozi wa dini wahakikishe wanatumia majukwaa ya nyumba za ibada kusisitiza wazazi na walezi wanawajibika kwa kiasi kikubwa kuisaidia serikali kuhakikisha hakuna mtoto aliyefaulu elimu ya msingi anabaki nyumbani.
MWISHO.
Comments
Post a Comment