DODOMA JIJI FC KIBARUANI DHITI YA MWADUI FC YA SHINYANGA

Na. Mwandishi Wetu,

TIMU ya Dodoma Jiji FC iliyo chini ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kesho Ijumaa Januari 1, 2021 siku ya mwaka mpya itakuwa kibaruani ugenini kwa mara nyingine kuikabili Mwadui FC ya Shinyanga kwenye dimba la Mwadui Complex majira ya saa 8:00 mchana katika mchezo wa kwanza wa mzunguko wa pili wa ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara.



Mchezo uliopita Dodoma Jiji iliitandika Mtibwa Sugar ya Morogoro bao 1-0 kwenye uwanja wa Jamhuri Manispaa ya Morogoro na sasa imehamishia makali hayo huko kwenye machimbo ya almasi ya Mwadui huku ari kikosini ikiwa juu kusaka pointi tatu za msingi.

Tayari kikosi cha wachezaji 20 na viongozi 8 kipo mkoani Shinyanga na leo Alhamisi Disemba 31 mchana kinatarajiwa kufanya mazoezi ya mwisho kwenye uwanja huo ili kuzoea hali ya hewa kwa sababu mchezo huo utaanza saa 8:00 mchana kwa majira ya Tanzania.

Dodoma Jiji FC imemaliza mzunguko wa kwanza ikiwa nafasi ya 8 kwenye msimamo wa ligi hiyo yenye timu 18 na inahitaji ushindi kwa udi na uvumba ili kuendelea kujiweka sehemu salama kwenye msimamo wa ligi hiyo wakati huu ambapo mshambuliaji wake Seif Abdallah Rashid Karihe akiwa amewasha moto kwenye kufumania nyavu akiwa amefunga katika michezo minne mfululuzo akiwa na magoli matano licha ya kusumbuliwa na majeraha na kukosa mechi za mwanzo wa msimu.

Wakati Karihe akitikisa nchi katika ufungaji, safu ya ushambuliaji itaongezewa makali na urejeo wa mshambulizi Anuar Jabiri ambaye alikuwa na majukumu ya nchi katika timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 20 maarufu Ngorongoro Heroes sambamba na beki wa kulia Anderson Solomoni.

 

MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.