Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bwana Gerald Kusaya amesema majukumu makubwa ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika ambayo ni udhibiti, usimamizi pamoja na uhamasishaji wa Vyama vya Ushirika hayawezi kutekelezwa ipasavyo bila ya kuwa na mifumo thabiti inayojengwa kwa vitendea kazi zikiwemo kompyuta na vyombo vya usafiri.
Katibu Mkuu Kusaya ameyasema hayo leo tarehe 31
Desemba, 2020 wakati akipokea kompyuta 100 za mezani (Desktop) kutoka kwa Benki
ya CRDB; Kompyuta hizo zimetolewa na Benki hiyo kama sehemu ya kuunga mkono
utendaji kazi wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika hususan eneo la usimamizi na
ukaguzi wa mara kwa mara wa Vyama vya Ushirika.
Katibu Mkuu Gerald Kusaya amepokea kompyuta hizo
100 zenye thamani ya shilingi milioni 150 Jijini Dodoma katika ofisi za Tume ya
Maendeleo ya Ushirika kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB
nchini Bwana Prosper Nambaya.
Katibu Mkuu Kusaya amesema kompyuta hizo 100
zitaongeza kasi na uwajibikaji ikiwa ni pamoja na kuongeza utoaji wa huduma kwa
Wanaushirika kote nchini pamoja na kuongeza ufanisi katika shughuli zote za usimamizi
wa Vyama vya Ushirika.
“Kompyuta hizi zinazokabidhiwa leo kwa Tume ya
Maendeleo ya Ushirika zitaongeza kasi ya uwajibikaji kwa Watumishi wa Tume
katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku katika kushughulikia maombi ya
leseni na utoaji wake kwa Vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo (SACCOS) kote
nchini”.
“Itakumbukwa kuwa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha
Na.10 ya Mwaka 2018 pamoja na Kanuni zake za Mwaka 2019, zinaelekeza kila Mtoa
huduma ndogo za fedha nchini zikiwemo SACCOS kutakiwa kuomba leseni kwa mujibu
wa sheria hiyo. Hivyo, kutolewa kwa kompyuta hizi kutasaidia Ofisi kusimamia
zoezi la utoaji wa leseni (ambazo zimekuwa zikiombwa na kutolewa kwa njia ya
mtandao – SACCOS Online Application System).”
“Kuongeza ufanisi na kasi katika utendaji kazi wa
shughuli za kila siku kwa Watumishi wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, ili
kuvisimamia kikamiifu Vyama vya Ushirika kwa njia za mifumo ya kiusimamizi”
“Kuongeza ufanisi katika upatikanaji, utunzaji na
utoaji wa taarifa na takwimu mbalimbali za Vyama vya Ushirika kama vile Idadi
ya Vyama, Wanachama, Hisa, Mtaji uzungukao, Ukaguzi, Usajili, Kesi na Migogoro,
Uwekezaji, Masoko, Madeni n.k.” Amekaririwa Katibu Mkuu Kusaya.
Naye Mrajis wa Ushirika nchini Dkt. Benson Ndiege
amesema msaada huo wa kompyuta kutoka kwa Benki ya CRDB utaongeza ufanisi
kutokana na Watumishi kadhaa wa Tume hiyo kukabiliwa na upungufu wa vitendea
kazi kama kopyuta pamoja na usafiri.
“Tume ya Maendeleo ya Ushirika kazi zetu zilikuwa
haziendi vizuri kutoakana na baadhi ya Wataalam kukosa vitendea kazi zikiwemo
kopyuta; Kuna Maafisa hawana kompyuta kabisa na hivyo kufanya kazi,
wanawasubiri wengine wawe wametoka au wawaombe pale amabapo hazitumiki.
Kutolewa wa kompyuta hizi kutaongeza tija kwenye majukumu yetu ya kila siku
yakiwemo ukusanyaji wa takwimu, kuratibu mafunzo, kufanya tafiti, kuratibu
uhamasishaji na nyingine.”
“Naomba kuwahakikishia Benki ya CRDB kuwa
tutaendelea kushirikiana nao katika shughuli za maendeleo ya Wananchi wetu.
Hasa pape Benki inayofanya biashara au kuwahudumia Wakulima kwa njia ya kutoa
mikopo na ushauri wa kifedha.”
“Tume kupitia Maafisa wake na Vyama vya Ushirika
watawasaidia kutoa taarifa za kutosha za Wakulima wanaotaka kukopeshwa na Benki
hii.” Amekaririwa Mrajis Mkuu Dkt. Benson Ndiege.
Naye Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa CRDB Bwana
Prosper Nabaya akiongea kwa naiba ya Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo amesema Benki
hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Maendeleo ya
Ushirika na kuongeza kuwa hadi sasa Benki hiyo imewakopesha Wakulima walio
kwenye Vyama vya Ushirika zaidi ya bilioni 650.
Bwana Prosper Nambaya ameongeza kuwa CRDB imekuwa
ndiyo Benki pekee inayofanya kazi za Wakulima wengi nchi kuliko Benki yoyote.
“Katika mwaka wa fedha wa 2019/20 Benki ya CRDB
imetoa jumla ya mikopo ya kilimo ya shilingi bilioni 650 sawa na asilimia 40%
ya mikipo yote ya kilimo nchini Tanzania.
Kati ya mikopo hiyo bilioni 495 imeelekezwa kwenye mazao makuu ya
kimkakati hivyo kumsaidia zaidi ya AMCOS 472 kupata mikopo kwa ajili ya
kuongeza tija kwenye uzalishaji wa kilimo (mikopo ya pembejeo, maghala, ujenzi
wa viwanda vya kuchakata mazao, mikopo kwa ajili ya miradi ya ufugaji,
uwekezaji kwenye misitu na mazao yake pia uwekezaji kwenye uvuvi.” Amekaririwa
Bwana Nambaya.
Bwana Nambaya amesema Benki ya CRDB imekuwa mstari
wa mbele katika kufufua Ushirika kwa kuongeza mitaji ili kuhuisha na kuujenga
Ushirika imara (TACOBA & KCBL).
“Benki ya CRDB inatoa mchango mkubwa kwa wana
ushirika kupitia mafunzo na misaada ya vifaa muhimu vya kufanyia kazi kama vile
kompyuta.”
“Tunatoa wito wa kuvikaribisha Vyama vyote vya Ushirika
nchini kujiunga na Benki ya CRDB ili viweze kujikwamua kiuchumi na kupata
mazingira wezeshi kwenye sekta zote za kiuchumi.” Amekaririwa Mkurugenzi
Nambaya.
Comments
Post a Comment