SANGA ATOA SIKU 60 KWA MAMLAKA YA MAJI SONGEA KUKAMILISHA MRADI

 



Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga ametoa Siku 60 kwa Mamlaka ya Majisafi  na Usafi wa Mazingira Songea (SOUWASA) kukamilisha ujenzi wa mradi wa maji wa kijiji cha Litisha katika Halmashauri ya wilaya ya Songea.

Mhandisi Sanga ameelekeza hayo Novemba 28, 2020 wakati wa ziara yake ya kukagua na kujionea hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa miradi ya maji inayotekelezwa wilayani humo akiwa ameambatana na Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama.

Akiwa kwenye mradi wa maji wa Litisha unaotekelezwa na wataalam wa ndani kutoka SOUWASA, Mhandisi Sanga alijionea hali halisi ya ujenzi wake ambapo alisema amefarijika kuona kisima kilichochimbwa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa kijiji hicho kikitoa maji mengi.

Hata hivyo alisisitiza ukamilishwe haraka na huku akikumbushia dhamira ya Serikali ya kuwasogezea huduma ya maji wananchi wakehasa wanyonge ili kuwapunguzia usumbufu wa kutembea umbali mrefu kufuatilia huduma ya magi.

“Nimefurahi kuonakisima kinatoa maji mengi sana na tenki tayari limekamilika lakini bado miundombinu ya kuwafikishia wananchi maji haijakamilika; maelekezo yangu ni kuwa, ndani ya siku 60 mradi huu uwe umekamilika na wananchi wawe wamepata huduma ya maji,” alielekeza Mhandisi Sanga.

Mhandisi Sanga aliwahakikishia wananchi wa Songea kwamba Serikali haitowaangusha, itahakikisha huduma ya majisafi na salama inawafikia wananchi mapema iwezekanavyo kama ilivyoahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu.

“Ninawahakikishia Serikali mliyoichagua kwa kura nyingi haitowaangusha, iliahidi na sasa inatekeleza, ni suala la muda tu, kero ya maji hapa Litisha na maeneo mengine ya jimbo hili la Peramiho tunakwenda kuimaliza,” alisisitiza Mhandisi Sanga.

Mhandisi Sanga alibainisha kwamba kabla ya mwezi huu kumalizika Wizara ya Maji itapeleka kiasi cha shilingi milioni 200 ili kuiwezesha SOUWASA kununua mabomba sambamba na kuhakikisha huduma ya nishati ya umeme imefika kwenye mradi ili wananchi wapate huduma.

“Tutaleta milioni 200 kwa ajili ya kununua mabomba na kujenga miundombinu ya kuwasogezea huduma wananchi wanyonge ili ndani ya siku 60, wawe wamefikishiwa maji,” alisisitiza Mhandisi Sanga.

Mhandisi Sanga alimpongeza Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama kwa jitihada zake za kufuatilia utekelezwaji wa miradi ya maji jimboni humo.

Akizungumzia utekelezaji wa miradi kwenye halmashauri ya wilaya ya Songea, Mkurugenzi Mtendaji wa SOUWASA, Mhandisi Patrick Kibasa alisema inatekelezwa kupitia Fedha za Mfuko wa Maji na inahusisha uchimbaji wa visima virefu na ujenzi wa miundombinu ya maji.

Kibasa alisema miradi inatekelezwa kwa awamu mbili tofauti na kwamba awamu ya kwanza inatekelezwa kupitia Mkandarasi Drilling and Dam Construction Agency (DDCA) na inahusisha uchimbaji wa visima virefu 39 katika vijiji 20 vya Halmashauri ya Wilaya ya Songea na kwamba tayari visima 19 vimechimbwa na shughuli inaendelea.

Aidha, aliongeza kuwa awamu ya pili inatekelezwa na wataalam wa ndani na inahusisha ujenzi wa miundombinu ya maji kwenye vijiji nane vilivyothibitika kuwa na maji ya kutosha na kwamba ujenzi umeanza katika vijiji vinne ambavyo ni Litisha, Litowa, Nakahuga na Peramiho B kwa gharama ya shilingi bilioni 2.4

MWISHO.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.