Na. Abdul Rahman Salim, RUKWA
Sheikh wa Mkoa wa Rukwa, Rashid Akilimali amekanusha uzushi unaoendelea
kusambazwa katika mitandao ya kijamii ukimuhusisha kuandika barua ya pongezi
kwenda makao makuu ya Baraza la Waislamu Tazania (BAKWATA) kwa jitihada za hali
na mali zilizofanywa na Baraza hilo kuhakikisha waislamu waliogombea nafasi za
uwakilishi wanashinda katika kura za maoni na hatimae kuteuliwa na Chama Cha
Mapinduzi (CCM).
Sheikh Akilimali alisema kuwa dhamira ya barua hiyo ni kuchafua na
kumdhalilisha na kuthibitisha kuwa yeye si muumini wa chama chochote cha siasa
isipokuwa kazi yake tangu kampeni za uchaguzi mkuu zianze ni kuhamasisha Amani
pamoja na kuwahubiria waumini kushiriki katika kupiga kura tarehe 28.10.2020 na
kumchagua mtu ambaye wanamuona atawaletea maendeleo katika jimbo lao nchi yao,
na mkoa wao kwa ujumla.
“Hivyo basi napenda kuwathibitiesheni kwamba barua hii, sikuiandika
mimi, haina saini yangu na wala haina hata nembo ya baraza kuu la waislamu wa
Tanzania, barua ambazo zinaandikwa na ofisi yet umara nyingi zinakuwa na nembo
yetu, zinakuwa na kumbukumbu namba na lazima zisainiwe na mtu aliyoiandika,
tunatoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Rukwa waelewe barua hii ni ya kumchafua
Sheikh Rashid Akilimali, barua iliyojaa ulaghai na uwongo mkubwa na si kweli
yaliyotamkwa ndani ya barua hii,” alisisitiza.
“Kama ni kuandika barua ningemu-address bosi wangu ambaye ni Mufti wa
Tanzania ndio ningempelekea barua, lakini barua haioneshi hivyo, inaonesha
inatoka ofisi ya mkoa inaelekea baraza kuu la Waislamu Tanzania, yaani hata
mwandishi mwenyewe hana maana na wala sio mtambuzi wa mambo na amejaribu
kunukuu aya za Qur’an ndani yake, aya zinazoleta mauaji na kidha wa kadha, vita
huu ni uchochezi ambao mimi binafsi na baraza langu la mashekhe mkoa wa Rukwa
hatulikubali,”
“Hivyo basi namtaka aliyoandika barua hii anitake radhi kabla
sijamchukulia hatua za kisheria na tayari nimekwishamtambua, ofisi yangu
imeshafanya uchunguzi, tumemtambua mwandishi wa barua hii, na baadhi ya
wanasiasa wanaitumia barua hii kuinadi kwaajili ya maslahi yao,” alisema.
Katika kusisitiza hilo Sheikh Akilimali ametoa siku 14 kwa mtu huyo kumuomba radhi na kuwaonya wanasiasa wote ambao wanaendelea kuinadi barua hiyo kwenye majukwaa yao ya kisiasa kuacha mara moja kwani wasipofanya hivyo atawachukulia hatua za kisheria.
MWISHO
Comments
Post a Comment