Kamati ya Amani Rukwa waipongeza NEC huku RC akionya watakaoleta vurugu

Na. Abdul Rahman Salim, RUKWA

Viongozi wa Kamati ya Amani Mkoani Rukwa Wameipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa utaratibu mzuri waliouweka katika vituo vya kupigia kura hali iliyopelekea kuondoa msongamano na wapiga kura kutimiza haki yao ya kikatiba bila ya bugudha wala kupoteza muda kwa kusimama kwenye foleni muda mrefu katika vituo hivyo.

Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akimsalimia Mwenyekiti wa Kamati ya Amani  Mkoa wa Rukwa Askofu Ambele Mwaipopo wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika.


Aidha, viongozi hao wametanguliza Shukrani zao kwa Mwenyezi  Mungu kwa kujalia hali ya utulivu na amani wakati wote wa kupiga kura na kuwashukuru Watanzania kwa kuzingatia maelekezo ya Tume katika muda wote wa zoezi hilo.

Akizungumza kwa niaba ya kamati hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Askofu Ambele Mwaipopo wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika alisema, “Tumeshuhudia katika vituo vyetu vya kupigia kura hali ikiwa shwari kabisa, na wapiga kura katika maeneo mengi nchini wameshuhudia kuwa kulikuwa na utengamano na utulivu mkubwa san ana tunawashukuru watanzania kwa kuzingatia maelekezo ya Tume mathalan, mara baada ya kupiga kura rudi nyumbani ili kupisha msongamano na karibu wote walifanya hivyo.”

Halikadhalika, Askofu Mwaipopo amewaomba watanzania kuendeleza utulivu wakati huu ambapo matokeo ya kura katika majimbo bado yanaendelea kutangazwa hadi pale wateule kwa nafasi ya Rais, Wabunge na Madiwani watakapokula nyapo zao.

“kikubwa ni kwamba baada ya haya matokeo kutangazwa, tuvunje makambi yetu ya kisiasa na kutoa ushirikiano kwa wale wote walioshinda na ikumbukwe kwamba, kwa nafasi ya Urais, iwe ama ulimchagua au la, ni Rais wako, vivyo hivyo kwa Wabunge na Madiwani, Ni uungwana na Uzalendo kwa Taifa letu kushikamana na kuwa wamoja kwaajili ya maslahi mapana ya nchi yetu,” Alisisitiza.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amewaasa waanchi wa mkoa wa Rukwa kuendeleza utulivu akiamini kuwa wanarukwa hawawezi kudanganywa na watu ambao wanadhamira ya kuanzisha vurugu baada ya kushindwa na kuwasihi kujikita kwenye masuala ya kilimo baada ya kumaliza zoezi la kuwachagua viongozi wawapendao.

“Kuna watu ambao kula yao ipo huko, akichochea ndio anaenda kula lakini wewe usipokwenda kulima hutakula, kwahiyo wanachi wawapuuze, hasa vijana, wawapuuze watu wote ambao wanataka kutuletea vurugu, lakini pili niwaonye wale wote wanaotaka kujaribu kutuvuruga ndani ya Rukwa wasijaribu, vyombo vya ulinzi na usalama viko macho sana, tuko vizuri mno tumejipanga, yeyote atakayeleta vurugu tutamshughulikia ipasavyo, tena kwa ukamilifu,” Alisisitiza.


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.