Na. Abdul Rahman Salim, RUKWA
Viongozi wa Kamati ya Amani Mkoani Rukwa
Wameipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa utaratibu mzuri waliouweka
katika vituo vya kupigia kura hali iliyopelekea kuondoa msongamano na wapiga
kura kutimiza haki yao ya kikatiba bila ya bugudha wala kupoteza muda kwa
kusimama kwenye foleni muda mrefu katika vituo hivyo.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akimsalimia Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Rukwa Askofu Ambele Mwaipopo wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Ziwa Tanganyika. |
Aidha, viongozi hao wametanguliza Shukrani zao kwa
Mwenyezi Mungu kwa kujalia hali ya utulivu na amani wakati wote wa kupiga
kura na kuwashukuru Watanzania kwa kuzingatia maelekezo ya Tume katika muda
wote wa zoezi hilo.
Akizungumza kwa niaba ya kamati hiyo Mwenyekiti wa
Kamati hiyo Askofu Ambele Mwaipopo wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Ziwa
Tanganyika alisema, “Tumeshuhudia katika vituo vyetu vya kupigia kura hali
ikiwa shwari kabisa, na wapiga kura katika maeneo mengi nchini wameshuhudia
kuwa kulikuwa na utengamano na utulivu mkubwa san ana tunawashukuru watanzania
kwa kuzingatia maelekezo ya Tume mathalan, mara baada ya kupiga kura rudi
nyumbani ili kupisha msongamano na karibu wote walifanya hivyo.”
Halikadhalika, Askofu Mwaipopo amewaomba watanzania
kuendeleza utulivu wakati huu ambapo matokeo ya kura katika majimbo bado
yanaendelea kutangazwa hadi pale wateule kwa nafasi ya Rais, Wabunge na
Madiwani watakapokula nyapo zao.
“kikubwa ni kwamba baada ya haya matokeo
kutangazwa, tuvunje makambi yetu ya kisiasa na kutoa ushirikiano kwa wale wote
walioshinda na ikumbukwe kwamba, kwa nafasi ya Urais, iwe ama ulimchagua au la,
ni Rais wako, vivyo hivyo kwa Wabunge na Madiwani, Ni uungwana na Uzalendo kwa
Taifa letu kushikamana na kuwa wamoja kwaajili ya maslahi mapana ya nchi yetu,”
Alisisitiza.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim
Wangabo amewaasa waanchi wa mkoa wa Rukwa kuendeleza utulivu akiamini kuwa
wanarukwa hawawezi kudanganywa na watu ambao wanadhamira ya kuanzisha vurugu
baada ya kushindwa na kuwasihi kujikita kwenye masuala ya kilimo baada ya
kumaliza zoezi la kuwachagua viongozi wawapendao.
“Kuna watu ambao kula yao ipo huko, akichochea ndio
anaenda kula lakini wewe usipokwenda kulima hutakula, kwahiyo wanachi
wawapuuze, hasa vijana, wawapuuze watu wote ambao wanataka kutuletea vurugu,
lakini pili niwaonye wale wote wanaotaka kujaribu kutuvuruga ndani ya Rukwa
wasijaribu, vyombo vya ulinzi na usalama viko macho sana, tuko vizuri mno
tumejipanga, yeyote atakayeleta vurugu tutamshughulikia ipasavyo, tena kwa
ukamilifu,” Alisisitiza.
Comments
Post a Comment