Na. Revocatus Kassimba, MOROGORO
Watumishi wa Wizara ya Kilimo wametakiwa kufanya
kazi kwa uadilifu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kuongeza tija
katika kuwahudumia wananchi.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya ametoa
wito huo leo (29.09.2020) mjini Morogoro wakati alipofungua mafunzo ya siku nne
kwa wakuu wa taasisi, bodi na wakala chini ya wizara kuhusu kamati za kudhibiti
uadilifu.
Kusaya amewataka watumishi wote kuwa waadilifu ndani
ya mioyo yao ili watende kazi walizokabidhiwa kama dhamana ya kuhudumia umma bila
upendeleo na kujiepusha na vitendo vya rushwa.
“Lengo la wizara ya kilimo ni kuwa na watumishi
wenye udilifu na maadili mema ndio maana nimetoa kibali mafunzo haya yafanyike
na kuwezesha kutimiza malengo ya kazi .Mtumishi mwadilifu atatumikia watanzania
muda wote “alisema Kusaya.
Mafunzo haya yanawakutanisha wakuu wa taasisi, bodi
za mazao na wakala pamoja na kamati za uadilifu toka taasisi zote 23 chini ya
wizara ya kilimo ambapo lengo ni
kujifunza namna ya kuishi uadilifu katika kuhakikisha shughuli za serikali
zinafikia malengo yaliyowekwa huku watumishi wakizingatia misingi ya uadilifu
na maadili.
Katibu Mkuu huyo wa wizara ya kilimo amewaambia watumishi hao kuwa katika utendaji kazi wao wanapimwa kwa matokeo hivyo wajibidiishe kutenda haki kwa wananchi pindi wawapo sehemu za kazi kwa kuepuka vitendo vinavyokiuka misingi ya maadili ikiwemo rushwa, kauli mbaya na matumizi mabaya ya madaraka.
“Tujione tunawiwa kuwahudumia watanzania kwani
tumepewa dhamana ya kuwatumikia wenzetu kwa uaminifu na uadilifu “Kusaya
alisema.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya uadilifu toka taasisi zote 23 chini ya wizara ya Kilimo yanayofanyika Morogoro |
Katika hatua nyingine Kusaya amesema atachukua
hatua kali kwa baadhi ya watumishi kwenye taasisi chini ya wizara ambapo
amebaini kuwa wanajihusisha na vitendo vibaya vya kuwajibu wananchi kwa kauli
mbaya.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Wakala Udhibiti
wa Viuatilifu (TPRI) Dkt. Magret Mollel amemshukuru Katibu Mkuu kwa kutoa
kibali cha kufanyika mafunzo hayo yenye kulenga kuongeza tija na utendaji kazi
wa wizara ya kilimo.
Dkt. Mollel alisema kwa siku nne wajumbe wa kamati
za uadilifu toka taasisi zote za wizara watashiriki mafunzo ya uadilifu na maadili
toka kwa wawezeshaji kutoka Ofisi ya Rais-Ikulu, Ofisi ya Rais Utumishi pamoja
na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Wizara ya Kilimo Filbert Lutare alisema mafunzo hayo yanahusisha washiriki 130 toka taasisi 23 chini ya wizara na kuwa wizara itahakikisha baada ya mafunzo haya watumishi kwenye taasisi zote wanaishi uadilifu na kuongeza kiwango cha maadili mema katika kuhudumia umma.
Aliongeza kusema kuwa Kamati za Kudhibiti Uadilifu
zinaundwa kwa mujibu wa Waraka wa Katibu
Mkuu Kiongozi wa mwaka 2017 ukilenga
kutekeleza Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa Awamu ya Tatu ili watumishi wa umma
washiriki kikamilifu na kwa vitendo kupambana na vitendo vya rushwa.
Mwisho
Comments
Post a Comment