Shinikizo la damu ni tatizo lenye idadi kubwa ya wagonjwa kwa asilimia 70 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Septemba 30, 2020 – Dar es Salaam
Na Mwandishi Maalum
Shinikizo la damu ni tatizo
linaloongoza kwa kushika namba moja kwa idadi kubwa ya wagonjwa katika Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambapo takwimu zinaonesha asilimia 70
wanakabiliwa na tatizo hilo.
Yalielezwa hayo jana na Daktari Bingwa
wa Magonjwa ya Moyo wa JKCI, Samweli Rweyemamu alipofanya mahojiano na
waandishi wa habari katika Viwanja vya Tanganyika Packers wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Moyo Duniani ambayo hufanyika Septemba 29, kila mwaka.
Dk. Rweyemamu alisema wapo pia wagonjwa
wengine wanaokabiliwa na tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu inayosambaza damu
kwenye moyo ambayo husababisha kifua kuuma.
“Kuna wengine wanaohitaji upasuaji
tunaona idadi inaongezeka kila siku, kwa mfano wale ambao mishipa ya damu
inaziba tunawazibua kwa upasuaji mkubwa (open heart surgery) au ule mdogo kwa
kutumia mtambo wa Cathlab.
“Tunaona wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji
wanaongezeka, mwaka jana hadi Desemba, kwa kutumia mtambo wa Cathlab tuliwachunguza
na kuwatibu wagonjwa 1409 hii ni idadi kubwa, wagonjwa hawa hapo
kabla tulikuwa tunawapa rufaa kwenda nje ya nchi,” alisema.
“Sasa hatujui kama wanaongezeka kwa sababu tunatangaza kila siku, wanajitokeza kuja hospitalini, tuna uwezo wa kuchunguza na kutibu, lakini kwa ujumla tunaweza kusema matatizo yameongezeka,” alisema.
Dk. Rweyemamu alitoa mfano, hivi
karibuni katika Wilaya ya Temeke, Viwanja vya Zakheem tulipima watu 103
asilimia 18 walikuwa na shinikizo la damu, wengine moyo umetanuka, kati yao wagonjwa
21 walionekana wana matatizo ya moyo.
“Tulienda pia Viwanja vya Mwembe Yanga
na kupima watu 150 asilimia 22 walionekana wana magonjwa ya moyo kati ya hiyo
asilimia 22, asilimia 19 walikuwa na shinikizo la damu la juu la damu,”
alisema.
Aliongeza “Utaona ni idadi ndogo
tunapima lakini tafiti zilizofanyika Dar es Salaam, zinaonesha karibu asilimia
30 wana shida ya shinikizo la damu, sasa ukiwa na shinikizo la damu ni ‘risk
factor’ ya kuziba kwa mishipa ya moyo kuziba hatimaye utafika katika Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) tukuzibue kwa vifaa maalum.
Dk. Rweyemamu alisema mtu akiwa na shinikizo la damu moyo hutanuka na kuwa na dalili za moyo kushindwa kufanya kazi (heart failure) kwa hiyo asilimia kubwa ya matatizo ya moyo kwa watu wazima yanaanza na shinikizo la damu.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa
JKCI, Prof. Mohamed Janabi alisema magonjwa ya moyo huchangia karibu asilimia
31 ya vifo vyote duniani na kwamba takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO)
zinaeleza kila mwaka takriban watu milioni 18 hufariki dunia kwa magonjwa hayo.
“Ni tatizo linaloonekana kuongezeka,
takwimu zinaonesha katika kila mwanamke mmoja kati ya wanne na mwanaume mmoja
kati ya watano wanakabiliwa na tatizo la shinikizo la damu,” alibainisha.
Aliongeza “Magonjwa ya moyo ni kati ya
magonjwa yasiyoambukiza, ambayo kinga ni rahisi kuliko tiba, ndiyo maana WHO
pamoja na Jumuiya ya Magonjwa ya Moyo Duniani baada ya kuona yanaongezeka
wakaamua kuanzisha Siku ya Moyo Duniani.
“Leo (jana) hapa tunaelimisha jamii
jinsi ya kujikinga, tunafanya uchunguzi na matibabu na wengine tunawapa rufaa
kuja kule kwenye taasisi yetu kwa matibabu zaidi.
“Watu wanapaswa kuzingatia unywaji wa
pombe kwa kiasi, kuacha uvutaji wa sigara, kula vyakula vinavyofaa, wazingatie
kunywa dawa wanazoandikiwa (waliokutwa na matatizo haya) na wafanye mazoezi,
wapunguze uzito uliopitiliza.
“Haya ni mambo ambayo yapo ndani ya
uwezo wa mtu bila gharama,” alisisitiza Prof. Janabi.
Mkurugenzi Mtendaji huyo alisema JKCI
kwa siku huwa wanaona takriban wagonjwa 300 hadi 400 na kwamba tangu wameanza
2015 hadi sasa tayari wameshaona wagonjwa 350,000 na kuwafanyia upasuaji wa
moyo wagonjwa 6,000.
“JKCI tupo mstari wa mbele kutoa elimu
ili watu waepuke magonjwa haya,” alisisitiza Prof. Janabi.
Awali, Mratibu wa Tiba wa Manispaa ya
Kinondoni kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Manispaa hiyo, Dk. Omary Mwangaza
alisema kipindi cha Julai na Agosti, mwaka huu katika vituo vya kutolea huduma
za afya, waliibua wagonjwa wapya zaidi ya 600 wanaokabiliwa na magonjwa
yasiyoambukiza.
“Shinikizo la damu na kisukari ni
magonjwa yaliyokuwa yakiongoza kwa idadi kubwa ya wagonjwa, wagonjwa wote hawa
tumewaingiza kwenye mfumo wetu wa matibabu,” alibainisha.
Alisema upimaji huo wa magonjwa ya moyo
bila malipo uliofanyika katika maadhimisho ya siku ya moyo Duniani umewasaidia
wananchi wengi kupata huduma kwani kuna ambao wamepewa dawa za kutumia, ushauri
na wengine rufaa za moja kwa moja kwenda kutibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete.
MWISHO
Comments
Post a Comment