Shinikizo la damu ni tatizo lenye idadi kubwa ya wagonjwa kwa asilimia 70 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)

Septemba 30, 2020 – Dar es Salaam

Na Mwandishi Maalum

Shinikizo la damu ni tatizo linaloongoza kwa kushika namba moja kwa idadi kubwa ya wagonjwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambapo takwimu zinaonesha asilimia 70 wanakabiliwa na tatizo hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akitoa elimu ya jinsi gani unaweza kuepuka kupata magonjwa ya moyo kwa wananchi waliofika katika viwanja vya Tanganyika Packers vilivyopo wilya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya siku ya moyo Duniani. Katika maadhimisho hayo wananchi walipata bila malipo huduma  za Upimaji,ushauri, matibabu ya moyo na rufaa ya moja kwa moja kwa wale waliokutwa na matatizo ya moyo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa


Yalielezwa hayo jana na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa JKCI, Samweli Rweyemamu alipofanya mahojiano na waandishi wa habari katika Viwanja vya Tanganyika Packers wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani ambayo hufanyika Septemba 29, kila mwaka.

Dk. Rweyemamu alisema wapo pia wagonjwa wengine wanaokabiliwa na tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu inayosambaza damu kwenye moyo ambayo husababisha kifua kuuma.

“Kuna wengine wanaohitaji upasuaji tunaona idadi inaongezeka kila siku, kwa mfano wale ambao mishipa ya damu inaziba tunawazibua kwa upasuaji mkubwa (open heart surgery) au ule mdogo kwa kutumia mtambo wa Cathlab.

“Tunaona wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji wanaongezeka, mwaka jana hadi Desemba, kwa kutumia mtambo wa Cathlab tuliwachunguza na kuwatibu wagonjwa 1409 hii ni idadi kubwa, wagonjwa hawa hapo kabla tulikuwa tunawapa rufaa kwenda nje ya nchi,” alisema.

Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Miraji akimpa ushauri wa lishe bora kwa afya ya moyo mwananchi aliyefika katika maadhimisho ya siku ya moyo Duniani yaliyofanyika jana kwenye viwanja vya Tanganyika Packers vilivyopo Kawe wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam. Katika maadhimisho hayo wananchi walipata bila malipo huduma za Upimaji,ushauri, matibabu ya moyo na rufaa ya moja kwa moja kwa wale waliokutwa na matatizo ya moyo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa

 “Sasa hatujui kama wanaongezeka kwa sababu tunatangaza kila siku, wanajitokeza kuja hospitalini, tuna uwezo wa kuchunguza na kutibu, lakini kwa ujumla tunaweza kusema matatizo yameongezeka,” alisema.

Dk. Rweyemamu alitoa mfano, hivi karibuni katika Wilaya ya Temeke, Viwanja vya Zakheem tulipima watu 103 asilimia 18 walikuwa na shinikizo la damu, wengine moyo umetanuka, kati yao wagonjwa 21 walionekana wana matatizo ya moyo.

“Tulienda pia Viwanja vya Mwembe Yanga na kupima watu 150 asilimia 22 walionekana wana magonjwa ya moyo kati ya hiyo asilimia 22, asilimia 19 walikuwa na shinikizo la damu la juu la damu,” alisema.

Aliongeza “Utaona ni idadi ndogo tunapima lakini tafiti zilizofanyika Dar es Salaam, zinaonesha karibu asilimia 30 wana shida ya shinikizo la damu, sasa ukiwa na shinikizo la damu ni ‘risk factor’ ya kuziba kwa mishipa ya moyo kuziba hatimaye utafika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) tukuzibue kwa vifaa maalum.

Dk. Rweyemamu alisema mtu akiwa na shinikizo la damu moyo hutanuka na kuwa na dalili za moyo kushindwa kufanya kazi (heart failure) kwa hiyo asilimia kubwa ya matatizo ya moyo kwa watu wazima yanaanza na shinikizo la damu.

Wananchi wakifanyiwa upimaji wa viashiria vya magonjwa ya moyo wakati wa maadhimisho ya siku ya moyo Duniani yaliyofanyika jana katika viwanja vya Tanganyika Packers vilivyopo  Kawe  wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam. Katika maadhimisho hayo wananchi walipata bila malipo huduma za Upimaji,ushauri, matibabu ya moyo na rufaa ya moja kwa moja kwa wale waliokutwa na matatizo ya moyo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Prof. Mohamed Janabi alisema magonjwa ya moyo huchangia karibu asilimia 31 ya vifo vyote duniani na kwamba takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaeleza kila mwaka takriban watu milioni 18 hufariki dunia kwa magonjwa hayo.

“Ni tatizo linaloonekana kuongezeka, takwimu zinaonesha katika kila mwanamke mmoja kati ya wanne na mwanaume mmoja kati ya watano wanakabiliwa na tatizo la shinikizo la damu,” alibainisha.

Aliongeza “Magonjwa ya moyo ni kati ya magonjwa yasiyoambukiza, ambayo kinga ni rahisi kuliko tiba, ndiyo maana WHO pamoja na Jumuiya ya Magonjwa ya Moyo Duniani baada ya kuona yanaongezeka wakaamua kuanzisha Siku ya Moyo Duniani.

“Leo (jana) hapa tunaelimisha jamii jinsi ya kujikinga, tunafanya uchunguzi na matibabu na wengine tunawapa rufaa kuja kule kwenye taasisi yetu kwa matibabu zaidi.

“Watu wanapaswa kuzingatia unywaji wa pombe kwa kiasi, kuacha uvutaji wa sigara, kula vyakula vinavyofaa, wazingatie kunywa dawa wanazoandikiwa (waliokutwa na matatizo haya) na wafanye mazoezi, wapunguze uzito uliopitiliza.

“Haya ni mambo ambayo yapo ndani ya uwezo wa mtu bila gharama,” alisisitiza Prof. Janabi.

Mkurugenzi Mtendaji huyo alisema JKCI kwa siku huwa wanaona takriban wagonjwa 300 hadi 400 na kwamba tangu wameanza 2015 hadi sasa tayari wameshaona wagonjwa 350,000 na kuwafanyia upasuaji wa moyo wagonjwa 6,000.

“JKCI tupo mstari wa mbele kutoa elimu ili watu waepuke magonjwa haya,” alisisitiza Prof. Janabi.

Awali, Mratibu wa Tiba wa Manispaa ya Kinondoni kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Manispaa hiyo, Dk. Omary Mwangaza alisema kipindi cha Julai na Agosti, mwaka huu katika vituo vya kutolea huduma za afya, waliibua wagonjwa wapya zaidi ya 600 wanaokabiliwa na magonjwa yasiyoambukiza.

“Shinikizo la damu na kisukari ni magonjwa yaliyokuwa yakiongoza kwa idadi kubwa ya wagonjwa, wagonjwa wote hawa tumewaingiza kwenye mfumo wetu wa matibabu,” alibainisha.

Alisema upimaji huo wa magonjwa ya moyo bila malipo uliofanyika katika maadhimisho ya siku ya moyo Duniani umewasaidia wananchi wengi kupata huduma kwani kuna ambao wamepewa dawa za kutumia, ushauri na wengine rufaa za moja kwa moja kwenda kutibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.

MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.