Veronica Simba – Ngara
Serikali
imewaasa wananchi wa Ngara, Mkoa wa Kagera kutunza miradi mbalimbali ya
maendeleo ya kijamii, inayoendelea kutekelezwa wilayani humo kupitia Mradi wa
kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Kagera (megawati 80).
Wito huo
ulitolewa jana Septemba 29, 2020 na Timu ya Serikali kutoka Tanzania
inayosimamia Mradi huo ikihusisha Wakurugenzi wa Bodi na Kamati ya Ufundi,
wakiwa katika ziara ya kazi yenye lengo la kukagua miradi mbalimbali ya kijamii
inayotekelezwa kupitia Mradi husika.
Akizungumza
kwa nyakati tofauti na Maafisa Watendaji pamoja na wananchi katika maeneo
mbalimbali kulipo na miradi hiyo, Kiongozi wa Timu hiyo, Mhandisi Innocent
Luoga ambaye ni Mjumbe wa Bodi wa Kamati husika, alisema endapo miundombinu
hiyo ya miradi husika isipotunzwa, itakuwa ni hasara kwa Serikali na wananchi
walengwa.
“Miradi hii
inayohusisha shule, vituo vya afya, miradi ya maji, miundombinu ya kilimo na
ufugaji bora inalenga kuwanufaisha wananchi, hivyo ili lengo hilo litimie,
inabidi itunzwe.”
Timu hiyo ikiwa
katika siku ya pili ya ziara yake, ilitembelea miradi kadhaa ikiwemo Shule ya
Msingi Makugwa iliyopo katika kijiji cha Mukubu ambayo imenufaika na Mradi huo
kwa kujengewa vyumba vya madarasa, Ofisi na nyumba za walimu, vyoo vya
wanafunzi pamoja na tanki la maji safi.
Mwalimu
Siyajali Manyasi ambaye ni Mkuu wa Shule hiyo aliueleza Ujumbe huo wa Serikali
kuwa, kujengwa kwa miundombinu hiyo kumeiwezesha Shule hiyo kupata usajili na
kujitegemea kutoka kuwa tawi la Shule ya Msingi Mukubu iliyoko umbali mrefu
kutoka hapo.
“Uwepo wa
Shule hii umewapunguzia watoto adha ya kutembea mwendo mrefu takribani kilomita
10 kwenda Mukubu na pia uwepo wa majengo haya ya kisasa umevutia wazazi wengi
zaidi kuwaleta watoto wao shuleni,” alisema Mwalimu Manyasi.
Vilevile, Timu
hiyo ilitembelea Shule ya Sekondari Bukiriro ambayo imenufaika kwa kujengewa
bweni la wanafunzi wa kike, bwalo la chakula na vyoo.
Aidha, Ujumbe
huo ulitembelea Chuo cha Ufundi Stadi Lemera kilichopo katika kijiji cha
Mukibogoye kilichonufaika kwa kujengewa karakana ya useremala na ushonaji nguo
pamoja na uwanja wa michezo ambao ujenzi wake unaendelea.
Timu
ilitembelea pia miradi ya kilimo cha kisasa kwa njia ya banda kitalu maarufu
kama ‘green house’ kwa lugha ya kigeni na mradi wa ufugaji nyuki, inayotekelezwa
katika kijiji cha Chivu, Kata ya Ntobeye, yote ikilenga kuwanufaisha wananchi
kiuchumi.
Akizungumza
katika ziara hiyo, Mratibu wa Miradi ya Maendeleo ngazi ya Wilaya, Herman Hume
alieleza kuwa miradi hiyo ya kijamii inayoendelea kutekelezwa wilayani Ngara
ilitengewa fedha kiasi cha dola milioni tano za Marekani ambazo ni sawa na
takribani shilingi bilioni 12 za Tanzania.
Kwa upande
wao, Mhandisi Salum Inegeja kutoka Wizara ya Nishati na Mhandisi Costa
Rubagumya kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ambao ni Wajumbe wa Kamati
ya Ufundi ya Mradi wa Rusumo, walikiri kurudhishwa na utekelezwaji wa miradi
hiyo lakini wakasisitiza umuhimu wa kuifanya iwe endelevu kwa maslahi ya
wananchi.
Katika ziara
hiyo, Timu ilifuatana pia na Mhandisi Patrick Lwesya, Meneja Mradi wa Rusumo,
Gaspar Mashingia, Afisa Mwandamizi, Jamii, Maendeleo na Uhamaji Makazi pamoja
na Maafisa kadhaa kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Ngara.
Mradi wa
Umeme Rusumo unatekelezwa kwa ushirikiano wa nchi tatu za Tanzania, Rwanda na
Burundi ambapo utakapokamilika unatarajiwa kuzalisha megawati 80 za umeme
zitakazogawanywa kwa nchi husika.
Comments
Post a Comment