“WAKULIMA WANAHITAJI MBOLEA YENYE UBORA NA BEI NAFUU” –KM KUSAYA

Na. Revocatus Kassimba, MANYARA

Serikali imeviagiza viwanda vya mbolea nchini kuzalisha mbolea yenye viwango vya juu vya ubora na kuiuza kwa wakulima kwa gharama nafuu ili uzalishaji wa mazao uwe na tija na kuchangia ukuaji wa uchumi.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw.Gerald Kusaya (kulia) akiongea na viongozi wa kiwanda cha mbolea cha Minjingu cha Manyara leo alipowatembelea kukagua uzalishaji.Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho Bw.Tosky Hans

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw. Gerald Kusaya ametoa kauli hiyo leo (28.08.2020) mkoani Manyara alipotembelea kukagua kiwanda cha mbolea cha Minjingu.

Alisema ameamua kufanya ziara kwenye mikoa iliyo na viwanda vya mbolea ili kuona namna wanavyozalisha ili kukidhi upungufu mkubwa wa mbolea ndani ya nchi hali inayopelekea wakulima kununua kwa bei kubwa.

“Nimeamua kufanya ziara hii kutembelea viwanda vya mbolea na kuongea na wazalishaji ili kuhamasisha upatikanaji wa mbolea yenye virutubisho bora na itakayouzwa kwa bei nafuu kwa wakulima nchini” alisema Kusaya.

Kusaya aliongeza kusema katika ziara zake nyingi mikoani alipokea malalamiko ya wakulima kuuziwa mbolea kwa bei kubwa na kutolea mfano mkoa wa Kagera alikuta mfuko wa kilo hamsini wa DAP ukiuzwa kati ya shilingi 80,000 hadi 90,000 kutokana na mbolea hiyo kuagizwa nje ya nchi.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw.Gerald Kusaya akiwa ameshika chupa ya mbolea ya maji (Booster) inayozalishwa na kiwanda cha Keen Feeders cha Arusha leo alipotembelea.Akiwa kiwandani hapo ameagiza bidhaa zote hizo zisajiliwe na kupata nembo ya ubora kabla hazijaingizwa sokoni ili kumlinda mkulima


“Lengo la serikali ni kumkomboa mkulima, lakini hatuwezi kufikia lengo hilo kama mbolea itaendelea kuuzwa kwa bei kubwa nchini.Ndio maana Tunataka viwanda vijengwe hapa nchini “ Kusaya alisema.

Katibu Mkuu huyo alisema mahitaji ya mbolea nchini ni takribani tani 664,000 wakati uzalishaji kwenye viwanda vyote 12 umefikia tani 38,000 pekee kwa mwaka.

Akizungumza kuhusu changamoto za kiwanda cha mbolea Minjingu kuwa na uzalishaji mdogo, Meneja Masoko wake Franks Kamhabwa alitaja tatizo la upatikanaji soko kukwamisha uzalishaji zaidi.

Kiwanda cha mbolea cha Minjingu kina uwezo wa kuzalisha tani 100,000 za mbolea kwa mwaka kutokana na akiba ya madini ya Phosphate takribani tani milioni 8 hadi 10 kwenye mgodi wake lakini sasa hivi wanazalisha tani 23,598 kwa mwaka.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw.Gerald Kusaya (kushoto ) akitoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa kiwanda cha Kahela Feeders cha Arusha Bw.Alex Kahela ( kulia) kuhakikisha anasajili bidhaa zake kwenye mamlaka za ubora ili zitambulike kwenye soko

Kamhabwa alitoa ombi kwa serikali kuwa kiwanda cha mbolea Minjingu kipewe fursa ya kupata soko la ndani ya nchi kupitia Mfumo wa Ununuzi wa Pamoja (BPS) sawa na mbolea zinazoagizwa nje ya nchi.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Minjingu Tosky Hans aliishukuru serikali kwa kukiunga mkono kiwanda hicho hali inayojidhihirisha kupitia Viongozi mbalimbali kuizungumzia vizuri mbolea ya Minjingu.

“Kiwanda hiki kilikuwa yatima huko nyuma, tunashukuru serikali ya Awamu ya Tano imetushika mkono kutusaidia bidhaa zetu sasa zinakubalika sokoni “alisema Hans.

Hans alimweleza Katibu Mkuu huyo wa Kilimo kuwa malengo ya kiwanda cha Minjingu ni kufikia uzalishaji wa tani 500,000 ifikapo mwaka 2025 na kuwa wataanzisha mashamba ya majaribio (Demo plots) katika halmashauri mbalimbali ili zitumike kufundishia wakulima juu ubora wa mbolea ya Minjingu.

Katika hatua nyingine Kusaya alitembelea viwanda vya kuzalisha mbolea za maji (Boosters) vya Kahela Feeders na Keen Feeders Ltd vya Arusha na kujionea hali ya uzalishaji bidhaa hiyo.

Akiwa katika kiwanda za mbolea Keen Feeders kilichopo Ngaramtoni Arusha alifahamishwa kuwa kiwanda hicho huzalisha lita 600,000 za mbolea ya maji na kuuzwa kwa wakulima hali inayosaidia kuongeza uzalishaji wa mazao.

Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw.Gerald Kusaya (kulia) akiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanda cha Minjingu cha Manyara  Bw.Tosky Hans (kushoto) leo alipotembelea kukagua hali ya uzalishaji wa kiwanda hicho ikiwa ni mkakati wa wizara ya Kilimo kuhamasisha viwanda vya ndani kuzalisha mbolea bora na yenye gharama nafuu kwa mkulima


Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho cha Keen Feeders Alfred Masawe alisema wanakutana na changamoto ya upatikanaji wa vifungashio na mitaji hali inayopelekea bei ya mbolea hiyo kuwa juu.

Katibu Mkuu Kusaya akiwa kwenye viwanda hivyo alibaini kuwepo kwa mapungufu ya bidhaa zinazozalishwa kutokuwa na nembo ya usajili wa ubora kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS)

Kusaya ameagiza wamiliki wa viwanda vyote ambavyo havina usajili wa Shirika la Viwango (TBS) pamoja na mamlaka zingine za udhibiti  kwenda kuomba leseni hizo ili wawe na uhakika wa soko na kulinda mazao ya wakulima na binadamu watakaotumia mazao yaliyozalishwa kwa mbolea hiyo aina ya Booster.

Kuhusu changamoto ya mitaji kwa wazalishaji wa mbolea za Booster ,Kusaya amewataka waende Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) na Mfuko wa Pembejeo nchini ( AGTIF) kukopa kwa kuwa ni taasisi za serikali na zinatoa riba nafuu kwa wakulima na wananchi.

“Nendeni TADB na AGTIF kukopa mitaji ya kukuza uzalishaji wa mbolea kwenye viwanda vyenu ili wakulima wapate mbolea hizo kwa gharama nafuu zaidi” alisema Kusaya.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA) Dkt. Stephano Ngailo (aliyesimama) akitoa maelezo kuhusu viwanda vya mbolea za maji leo katika kiwanda cha Keen Feeders Arusha.Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.Gerald Kusaya  alitembelea kiwanda hicho (katikati) na kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda cha Keen Feeders Bw.Alfred Massawe.Kiwanda hicho huzalisha lita  600,000 za mbolea maji (boosters) kwa mwaka


Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA) Dkt. Stephano Ngailo aliyeambatana na Katibu Mkuu kwenye ziara hiyo amemshukuru kwa kazi kubwa aliyoifanya kutembelea na kuhamasisha wazalishaji mbolea kwenye mikoa mitano.

Dkt. Ngailo alisema amepokea malekezo yote ya serikali yaliyotolewa na Katibu Mkuu na kuwa watahakikisha wazalishaji wa mbolea nchini kote wanazingatia ubora na kuuza bidhaa hizo kwa gharama nafuu ili iwafikie wakulima wengi.

Kusaya pia ameagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA) kufanya ukaguzi wa mbolea zisizo na viwango (fake) ambazo zinalalamikiwa na wazalishaji wadogo kuwa zinaharibu soko lao kwa kuuzwa mitaani.

“ TFRA fuatilieni mbolea (booster) zisizo na ubora kwenye masoko ya Kariakoo, Arusha, na kwingineko  mikoani na kuchukua hatua kali za kisheria kwa wauzaji na watengenezaji ili kudhibiti  zisiendelee kusambaa.Nipate taarifa yenu ya utekelezaji mapema.” aliagiza Katibu Mkuu Kusaya akiwa Arusha.

Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Kilimo amehitimisha ziara yake ya kutembelea viwanda vya mbolea na kukutana na wazalishaji katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara ambapo imemwezesha kujionea hali halisi ya uzalishaji na upatikanaji mbolea nchini.

 

Mwisho.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.