CHUO KIKUU CHA USHIRIKA MOSHI FANYENI TAFITI KUBORESHA UTENDAJI KAZI WA VYAMA VYA USHIRIKA – KM KUSAYA
Na. Revocatus Kassimba, MOSHI
Wizara ya Kilimo imekitaka Chuo Kikuu cha Ushirika
Moshi (MoCU) kuwa na utaratibu wa kufanya utafiti kujua namna ambavyo jamii ya
watanzania inanufaika na ushirika nchini ili kiboreshe mitaala yake ya
kufundishia.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Bw. Gerald Kusaya ametoa rai hiyo leo alipozungumza na Menejimenti ya Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi baada ya kukitembelea ikiwa ni sehemu ya ziara yake kukagua utendaji kazi wa taasisi zinazofanya kazi ya kuinua sekta ya kilimo nchini.
Alisema chuo hicho kina mchango mkubwa katika
kuifanya sekta ya ushirika nchini kuchangia ukuaji wa uchumi na kuwezesha wana
ushirikia kunufaika na kazi zao kupitia mafunzo yanayotolewa kwa wataalam.
“Nendeni kwenye vyama vya ushirika na AMCOS
kuangalia namna wanavyotekeleza majukumu yao na kuwapa mafunzo ya kuboresha ili
ushirika uwe na mchango katika kukuza kilimo na pato la wakulima” alisema
Kusaya.
Kusaya amekitaka pia chuo Kikuu cha Ushirika Moshi kuanzisha ushirikiano wa karibu na Tume ya
Maendeleo ya Ushirika (TCDC) pamoja na Shirika la Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika
(COASCO) zilizo chini ya Wizara ya Kilimo kufundisha wana ushirika wakiwemo
watumishi ili sekta hiyo iweze kusaidia ushirika kuondokana na kero za
ubadhirifu na usimamizi mbaya wa mali za wakulima.
Ili kufika lengo la kufanya watendaji wa vyama vya
ushirika wawe na weledi na ujuzi Katibu Mkuu huyo ametoa wito kwa chuo
kuanzisha utaratibu wa kuwapanguia wanafunzi wake kwenda kufanya mafunzo kwa
vitendo kwenye vyama vya ushirika na AMCOS kote nchini kuanzia mwaka huu.
“Wanafunzi wanosoma hapa tutawapa nafasi ya kwenda
kufanya mafunzo kwa vitendo kwenye vyama vyetu vya Ushirika ili wasaidie kuimarisha
utendaji kazi wa ushirika hali itakayowapa pia watumishi wa vyama hivyo weledi “alisema
Katibu Mkuu Kusaya.
Katika hatua nyingine Kusaya alisema wizara yake
inatekeleza agizo la Waziri Mkuu la kuhakiksha vyama vya ushirika vinaongozwa
na watendaji wenye sifa na weledi wa ushirika ili kuondoa tatizo la ubadhirifu
na utendaji mbovu ambapo kwa kuanzia wataajiliwa Mameneja Wakuu wa Vyama vikuu
vya Nyanza, Shirecu na KCU.
Akitoa taarifa ya chuo Kikuu cha Ushirika Moshi, Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Alfred Sife alisema chuo kimeendelea kuwa na mafanikio katika kufundisha taaluma ya ushirika nchini na wanafunzi wengi wamenufaika baada ya kuhitimu.
Alisema pia kazi kubwa chuo Kikuu cha ushirika
Moshi inachokifanya ni kuzalisha rasilimali watu wanaoweza kuendesha vyama vya
Ushirika na kushiriki katika uchumi wa nchi.
“Chuo chetu kinazalisha wataalam wengi lakini
ukienda katika vyama vya ushirika huko kwenye jamii huwakuti ndio maana utakuta
taarifa nyingi za ukaguzi wa hesabu na mali za ushirika zinazotolewa na COASCO
zinaonyesha uwepo wa tatizo la utunzaji hesabu” alisema Prof. Sife.
Prof. Sife aliongeza kusema anaomba Wizara ya
Kilimo ambayo kwa kiwango kikbwa ndio yenye vyama vya ushirika kutokana na
sekta ya Kilimo kushirikiana na chuo kutoa mafunzo ya muda mufupi kwa watendaji
na viongozi wa ushirika ili waweze kutekleza majukumu yao kwa weledi na kufanya
ushirika wa kisayansi na kutumia teknolojia rahisi ikiwemo mfumo wa upatikanaji
tawimu sahihi za wana ushirika na manufaa wanayopata kiuchumi.
Kwa mujibu wa Makamu Mkuu huyo alisema chuo hicho
katika mwaka wa masomo 2020/21 kina wanafunzi 7,231 waliopo kwenye program zaidi
ya 36 zinazofundishwa chuoni hapo huku kikiwa na idadi ya watumishi 338 tangu
kilipoanzishwa mwaka 2014.
Awali leo Katibu Mkuu Kusaya alikutana na kufanya
mazungumzo na Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro, Dkt. Khatibu Kazungu kuhusu
mwenendo na changamoto za sekta ya kilimo kwenye Mkoa huo.
Katibu Mkuu yuko mkoani Kilimanjaro kwa ziara ya
kukagua uetendaji kazi wa taasisi chini ya wizara na kufanya ufuatiliaji wa
viwanda vya kuzalisha mbolea nchini.
Mwisho
Comments
Post a Comment