WAZIRI SIMBACHAWENE AITAKA POLISI KUKAA MGUU SAWA UCHAGUZI MKUU, AIPONGEZA RUFIJI KUSAMBARATISHA WAHALIFU


Na. Mwandishi Wetu, MOHA, RUFIJI

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene amelitaka Jeshi la Polisi kudhibiti vurugu zozote au uvunjifu wa sheria hasa katika kipindi hiki nchi inapoelekea katika uchaguzi mkuu.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene akimpa maelekezo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Rufiji, SAP Onesmo Lyanga (kulia), wakati alipofanya ziara Ofisi ya Kamanda huyo, Mjini Ikwiriri, Wilaya ya Rufiji, leo. Kushoto ni Mkuu wa Utawala wa Mkoa huo, ACP Richard Ngole. Amelitaka Jeshi hilo kudhibiti vurugu zozote au uvunjifu wa sheria hasa katika kipindi hiki nchi inapoelekea katika uchaguzi mkuu
Amewataka muda wote wawe tayari kwa kujipange vizuri na pia intelejensia wahakikishe kila kinachotekea katika jamii wanakijua ili kuhakikisha nchi inakua salama na uchaguzi umalizike salama.

Akizungumza na Viongozi Wakuu wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, Mjini Ikwiriri leo, wakati alipokuwa safarini akitokea Mkoani Mtwara kuelekea Jijini Dar es Salaam, Simbachawene amewataka Polisi wasije kujisahau na kudhani kuwa wapo salama sana bali muda wote wawe macho kujilinda, kulinda raia na mali zao.

“Msije mkajisahau mkadhani mpo salama sana, hawa watu uvamia pale mnapojisahau ndipo wanafanya hayo mambo. Tunapoelekea kipindi hiki cha uchaguzi ni vizuri mkawa katika tahadhali, intelejensia ikae vizuri kuhakikisha kila kinachotokea kwenye jamii mnakijua,” alisema Simbachawene.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene (katikati), akimsikiliza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Rufiji, SAP Onesmo Lyanga (kulia), wakati akitoa taarifa ya hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa wake. Waziri huyo alifanya ziara Ofisi ya Kamanda huyo, Mjini Ikwiriri, Wilaya ya Rufiji, leo, na kuwataka Polisi kudhibiti vurugu zozote au uvunjifu wa sheria katika kipindi hiki cha uchaguzi mkuu. Kushoto ni Mkuu wa Utawala wa Mkoa huo, ACP Richard Ngole
Aliongeza kuwa, “Mshirikiane na vyombo vingine kudhibiti uhalifu, Serikali ni moja, dola ni moja, Mamlaka ni moja na Amiri Jeshi Mkuu ni mmoja, kwahiyo pale mnapopungukiwa tumia taarifa kutoka kwa wenzenu.”

Pia Simbachawene alilitaka Jeshi hilo lithibiti matukio ya uhalifu kuanzia chini na pia wasilipuuze kwa kuwa tukio likidharauliwa ndipo baadaye linbakuja kuwa kubwa na kuleta matatizo makubwa katika jamii.

“Mdhibiti matukio kuanzia chini, utakuta tukio lina cheni fulani lakini halishughulikiwi, hivyo linazaa lingine na matokeo yake linakua kubwa zaidi, matukio yanayotokea yathibitiwe kwa kiasi cha kutosha ili yasije kuleta madhara makubwa hapo baadaye,” alisema Simbachawene.

Aidha, Waziri huyo aliahidi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, ambapo atahakikisha anamfikishia ombi Rais, Dkt. John Pombe Magufuli aweze kusaidia kuanza kwa ujenzi wa ofisi hiyo.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene (kushoto), akisalimiana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Rufiji, SAP Onesmo Lyanga, wakati alipokua anawasili Ofisi ya Kamanda huyo, Mjini Ikwiriri, Wilayani Rufiji, leo. Kulia ni Mkuu wa Utawala wa Mkoa huo, ACP Richard Ngole
“Nitamuomba mheshimiwa Rais aone uharaka wa kutupa fedha ya ujenzi wa ofisi, ambayo ni shilingi milioni mia tatu, bila ofisi mnawezaje kufanya kazi, hatuwezi kuwaacha watu kwenye vijumba vyenye joto, itakua ni mateso, tutajitahidi tuweze kufanikisha hili kwa kulifanyia kazi kwa uharaka zaidi,” alisema Simbachawene.

Waziri huyo pia alimpongeza Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa kipolisi pamoja na wasaidizi wake, kuhakikisha wanadhibiti uhalifu kwa kiasi kikubwa na sasa eneo hilo lina amani na wananchi wanaendelea na shughuli zao za maendeleo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa Kipolisi, SACP Onesmo Lyanga alisema Mkoa wa Kipolisi Rufiji hali ya usalama imeimarika na Wilaya zote nne za Kiserikali ambazo ni Rufiji, Kibiti, Mkuranga na Mafia zipo salama.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene (kushoto), akiangalia ramani ya ujenzi wa Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Rufiji, ambayo inahitajika shilingi milioni mia tatu ili iweze kujengwa. Waziri huyo aliahidi kuzitafuta fedha hizo ili kufanikisha ofisi hiyo iweze kujengwa. Kulia ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, SAP Onesmo Lyanga. Simbachawene alifanya ziara katika ofisi hizo zilizopo Ikwiriri, Wilayani Rufiji, leo
“Mkoa huu wa Kipolisi ulianzishwa mwaka 2017, na mpaka sasa, hali ya uhalifu ni shwari, tunaendelea kufanya misako na doria kupambana na uhalifu mdogo na mkubwa unaofanyika katika Mkoa wa Kipolisi Rufiji,” alisema Lyanga.

Pia Lyanga alimshukuru Waziri huyo kwa kuwatembelea, na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote aliyowapa, na wataendelea kufanya kazi kwa weledi muda wote kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama katika Mkoa huo.

Mwisho

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.