WAZIRI SIMBACHAWENE AITAKA POLISI KUKAA MGUU SAWA UCHAGUZI MKUU, AIPONGEZA RUFIJI KUSAMBARATISHA WAHALIFU
Na. Mwandishi Wetu,
MOHA, RUFIJI
WAZIRI
wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene amelitaka Jeshi la Polisi
kudhibiti vurugu zozote au uvunjifu wa sheria hasa katika kipindi hiki nchi
inapoelekea katika uchaguzi mkuu.
Amewataka
muda wote wawe tayari kwa kujipange vizuri na pia intelejensia wahakikishe kila
kinachotekea katika jamii wanakijua ili kuhakikisha nchi inakua salama na
uchaguzi umalizike salama.
Akizungumza
na Viongozi Wakuu wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, Mjini Ikwiriri leo, wakati
alipokuwa safarini akitokea Mkoani Mtwara kuelekea Jijini Dar es Salaam,
Simbachawene amewataka Polisi wasije kujisahau na kudhani kuwa wapo salama sana
bali muda wote wawe macho kujilinda, kulinda raia na mali zao.
“Msije
mkajisahau mkadhani mpo salama sana, hawa watu uvamia pale mnapojisahau ndipo
wanafanya hayo mambo. Tunapoelekea kipindi hiki cha uchaguzi ni vizuri mkawa
katika tahadhali, intelejensia ikae vizuri kuhakikisha kila kinachotokea kwenye
jamii mnakijua,” alisema Simbachawene.
Aliongeza
kuwa, “Mshirikiane na vyombo vingine kudhibiti uhalifu, Serikali ni moja, dola
ni moja, Mamlaka ni moja na Amiri Jeshi Mkuu ni mmoja, kwahiyo pale
mnapopungukiwa tumia taarifa kutoka kwa wenzenu.”
Pia
Simbachawene alilitaka Jeshi hilo lithibiti matukio ya uhalifu kuanzia chini na
pia wasilipuuze kwa kuwa tukio likidharauliwa ndipo baadaye linbakuja kuwa
kubwa na kuleta matatizo makubwa katika jamii.
“Mdhibiti
matukio kuanzia chini, utakuta tukio lina cheni fulani lakini halishughulikiwi,
hivyo linazaa lingine na matokeo yake linakua kubwa zaidi, matukio yanayotokea
yathibitiwe kwa kiasi cha kutosha ili yasije kuleta madhara makubwa hapo
baadaye,” alisema Simbachawene.
Aidha,
Waziri huyo aliahidi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo
ukosefu wa ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, ambapo
atahakikisha anamfikishia ombi Rais, Dkt. John Pombe Magufuli aweze kusaidia
kuanza kwa ujenzi wa ofisi hiyo.
“Nitamuomba
mheshimiwa Rais aone uharaka wa kutupa fedha ya ujenzi wa ofisi, ambayo ni
shilingi milioni mia tatu, bila ofisi mnawezaje kufanya kazi, hatuwezi kuwaacha
watu kwenye vijumba vyenye joto, itakua ni mateso, tutajitahidi tuweze kufanikisha
hili kwa kulifanyia kazi kwa uharaka zaidi,” alisema Simbachawene.
Waziri
huyo pia alimpongeza Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa kipolisi pamoja na
wasaidizi wake, kuhakikisha wanadhibiti uhalifu kwa kiasi kikubwa na sasa eneo
hilo lina amani na wananchi wanaendelea na shughuli zao za maendeleo.
Kwa
upande wake Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa Kipolisi, SACP Onesmo Lyanga
alisema Mkoa wa Kipolisi Rufiji hali ya usalama imeimarika na Wilaya zote nne
za Kiserikali ambazo ni Rufiji, Kibiti, Mkuranga na Mafia zipo salama.
“Mkoa
huu wa Kipolisi ulianzishwa mwaka 2017, na mpaka sasa, hali ya uhalifu ni
shwari, tunaendelea kufanya misako na doria kupambana na uhalifu mdogo na
mkubwa unaofanyika katika Mkoa wa Kipolisi Rufiji,” alisema Lyanga.
Pia
Lyanga alimshukuru Waziri huyo kwa kuwatembelea, na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo
yote aliyowapa, na wataendelea kufanya kazi kwa weledi muda wote kwa
kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama katika Mkoa huo.
Mwisho
Comments
Post a Comment