Wananchi wameshauriwa kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara na kuwa na bima aa afya ambayo itawasaidia pindi watakapuuguwa
Wataalamu wa magonjwa wa moyo wakiangalia maendeleo ya aliyekuwa Mbunge wa Nzega Mhe. Lucas Lumambo Selelii aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo na kupandikiza mshipa wa damu kwenye moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Na. Mwandishi
Wetu, DAR ES SALAAM
Wananchi
wameshauriwa kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara kwa kufanya hivyo
watatambua kama wana maradhi au la na kama wana maradhi wataweza kupata
huduma za matibabu kwa wakati.
Pia wameombwa
kuwa na bima ya afya ambazo zitawasaidia kupata matibabu pindi
watakapouguwa kwani maradhi huja muda wowote, wakati wowote na mahala
popote bila ya kupiga hodi.
Rai hiyo
imetolewa hivi karibuni na aliyekuwa Mbunge wa Nzega Mhe. Lucas
Lumambo Selelii aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo na kupandikiza
mshipa wa damu kwenye moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Akizungumza kwa
furaha na mwandishi wa habari hii Mhe. Selelii alisema huduma
za matibabu ya moyo ya kibingwa ambayo hapo awali yalikuwa yakipatikana nje ya
nchi sasa yanapatikana hapa nchini kwa kiwango cha juu kupitia madaktari
wabobezi na wataalam wa upasuaji wa moyo.
“Matibabu
niliyoyapata pamoja na mengine yanatotolewa katika Taasisi hii yanatokana na
jitihada zilizofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
kuwekeza vifaa tiba vya matibabu ya kibingwa ya magonjwa ya moyo ili
kuwawezesha wananchi wa matabaka yote kupata huduma hapa nchini.
“Namshukuru
Mwenyezi Mungu, upasuaji mkubwa wa moyo wa kuvuna mshipa wa damu kutoka kwenye
mguu na kuupandikiza katika moyo ulifanyika vizuri na hivi leo ninavyoongea
kama mnavyoniona maumivu yote niliyokuwa nayo mwanzo yameacha na ninajisikia
vizuri,” alisema Mhe Selelii.
Mhe. Selelii
alisema kabla ya kufanyiwa upasuaji huo alianza kusikia moyo unapata vichomi
maumivu ambayo yalikuwa yakienda hadi mgongoni, ni ugonjwa ambao hakuwahi
kuugua katika maisha yake.
“Nilikuja Dar
es Salaam kwa ajili ya mambo yangu binafsi lakini ghafla nikiwa hotelini usiku
ndio nikaanza kupata maumivu ambayo yalinifanya niamke asubuhi na mapema kwenda
hospitali kwa ajili ya matibabu,”
“Vipimo vya
awali vilionesha nina shinikizo la juu la damu la 170 kwa 120, na kushauriwa
nitumie dawa za presha, baada ya kuwasiliana na ndugu na jamaa kuhusu hali
niliyokutwa nayo walinishauri nifike hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa
ajili ya uchunguzi zaidi,” alisema Mhe Selelii.
Baada ya
kufanyiwa vipimo katika hospitali ya Muhimbili ilionekana kuwa na viashiria vya
magonjwa ya moyo hivyo kufikishwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
kwa ajili ya vipimo zaidi na matibabu.
“Kwakuwa
sijawahi kuugua toka kuzaliwa kwangu, sikuwahi kukata bima ya afya, hivyo
nilivyoambiwa nina tatizo la moyo niende JKCI niliwakatalia na kuwaambia sina
hela wala bima ya afya, nashukuru wahudumu wa afya walinishawishi na kuniambia
hela hutafutwa lakini maisha huwezi kuyatafuta mara ya pili hivyo ni vyema
kufanyiwa uchunguzi wa kina ili ijulikane unanatizo gani,”
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Rosemary Mpella
akimpima shinikizo la damu mwilini (BP) aliyekuwa Mbunge wa Nzega Mhe. Lucas
Lumambo Selelii aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo na kupandikiza
mshipa wa damu kwenye moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
“Nimefurahia
kwa huduma ya upasuaji wa moyo niliyoipata hapa JKCI maana waliniandaa na
kuniambia kila kitu nitakachofanyiwa katika upasuaji huo na hivyo kunifanya
kuwa tayari kufanyiwa upasuaji bila uoga wowote”, alizungumza kwa furaha Mhe.
Selelii.
Kwa upande wake
daktari bingwa wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Evarist
Nyawawa alisema walimpokea Mhe. Selelii akiwa na matatizo ya kushindwa kupumua
na kuishiwa nguvu, ambapo baada ya vipimo ilionekana mishipa mitatu ya damu
inayopeleka damu katika misuli ya moyo kuziba.
“Upasuaji
tuliomfanyia ni wa kuvuna mishipa ya damu kutoka katika miguu na kuipandikiza
kwenye moyo, upasuaji huu umechukua masaa matano na baada kufanikisha
matibabu hayo mgonjwa tulimuhamishia katika chumba cha uangalizi maalum (ICU)
baada ya hali yake kuimarika alipelekwa wodini na anaweza kuruhusiwa siku
yoyote kuanzia sasa”, alisema Dkt. Nyawawa.
Upasuaji
uliofanyika ni wa kuvuna mshipa mkubwa wa damu kutoka kwenye mguu na ndani ya
kifua na kuipandikiza juu ya mishipa ya damu ya moyo
iliyokuwa imeziba ili kuifanya damu iweze kupita vizuri (Coronary
Artery Bypass Grafting -CABG).
Mwisho
Comments
Post a Comment