Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais , Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt Dorothy Gwajima.
Na. Majid Abdulkarim, Dar es Salaam
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia maswala ya Afya, Dkt.
Dorothy Gwajima ametoa wito na kuwasisitiza watumiaji wote wa huduma za afya
nchini katika zahanati, vituo vya afya na hospitali za halmashauri kutumia
namba za huduma kwa wateja zilizopo katika vituo hivyo ili kuwasilisha kero zao
mahali sahihi na kupatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Dkt. Gwajima ametoa wito huo leo Jijini Dar es
Salaama akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua uimarishaji mfumo wa
huduma kwa wateja katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na Hospitali ya Sinza
Palestina .
Aidha Dkt Gwajima amesema, mahala sahihi pa
kuripoti Kero za Wateja wakati wa kupata huduma ni kwa Mganga Mkuu wa Kituo,
Mganga Mkuu wa Halmashauri, Mganga Mkuu wa Mkoa, Ofisi ya Rais TAMISEMI na
ikishindikana hapo Wizara ya Afya.
“ Ili kurahisisha kero hizo kufika kwa wakati
kila kituo cha kutolea huduma za afya (zahanati, kituo cha afya na
hospitali ya Halmashauri) sasa kinatekeleza kuimarisha mfumo mzima wa huduma kwa
wateja kwa kutumia utaratibu wa kuweka namba za simu kwenye enao la wazi
linaloonekana hususani pale wanapokaa wateja kusubiria huduma hivyo, wateja
wahakikishe wanapata namba hizo na kuzitumia ili kusaidiwa kwa wakati”,
amesisitiza Dkt. Gwajima.
Dkt. Gwajima amesema kuwa Wito huo
umekuja baada ya kubaini uwepo wa matukio ya baadhi ya watumiaji wa
huduma za afya katika baadhi ya vituo kulalamikia kero walizokutana nazo wakati
wa kupata huduma za afya huku muda mrefu ukiwa umepita hivyo, kukosa fursa ya kupata
ufumbuzi kwa wakati.
Lakini pia Dkt Gwajima amewaagiza Waganga
Wakuu wa Mikoa na Halmashauri zote nchini ndani ya siku saba kuhakikisha mfumo
huu unaimarishwa mara moja na taarifa zinawafikia wananchi wote waanaotumia
huduma katika maeneo husika.
Kwa kuongezea Dkt. Gwajima amesema kuwa, kila
zahanati, kituo cha afya na hospitali ya Halmashauri lazima iwe na bango kubwa
lenye kuonesha namba maalumu ya simu ya kituo kwa ajili ya kushughulikia kero
za wateja wanaokuja kupata huduma za afya vilevile, namba ya Mganga Mfawidhi wa
Kituo husika, namba ya Mganga Mkuu wa Halmashauri, Mganga Mkuu wa Mkoa, namba
za Ofisi ya Rais TAMISEMI na namba ya Kituo maalumu cha Simu (Call Centre) cha
Wizara ya Afya ambayo ni 199.
“Na sisi kama Ofisi ya Rais TAMISEMI leo tunatangaza
namba maalumu ya kupokea Kero na Pongezi kutoka kwa wateja juu ya utoaji huduma
za afya katika hospitali zetu za ngazi ya afya ya msingi na namba hiyo ni
0734124191. Hivyo, iwapo Mteja utakuwa na Kero na hujapata msaada ngazi ya
kituo, mganga mkuu wa halmashauri na mkoa basi usiondoke na kero yako bali
haraka tuma ujumbe juu ya kero hiyo ukieleza uko Halmashauri gani na Kituo gani
na sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI tutakupigia na kuchukua hatua stahiki za kupata
ufumbuzi juu ya kero hiyo kwa wakati sahihi” ameeleza Dkt. Gwajima.
Dkt. Gwajima amebainisha kuwa lengo la
kuimarisha huduma kwa Wateja ni kutatua kero zao kwa wakati na kuhakikisha kila
mwananchi anayefika kwenye kituo cha huduma za afya ngazi ya msingi anafurahia
huduma hizo na haondoki huku moyoni akiwa na manung’uniko yasiyo ya lazima.
Katika hatua nyingine Dkt. Gwajima
amewapongeza wataalamu wa sekta ya afya nchini kwa kupokea kwa uzalendo na
kutekeleza kwa vitendo mwelekeo wa kupambana na kudhibiti ugonjwa wa Covid 19
kupitia maono makubwa ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John
Pombe Magufuli kuwa.
“tuwe wabunifu na tupigane vita hii bila hofu
na kwa kuzingatia mazingira mahsusi ya nchi yetu, Kupitia maono haya Covid 19
imedhibitiwa mapema sana na Tanzania imeandika historia duniani juu ya mbinu za
ubunifu na uzalendo juu ya mapambano haya”ameeleza Dkt.Gwajima.
Dkt Gwajima amesema, jukumu liliko mbele ya
wataalamu wa huduma za afya nchini ni kuimarisha utekelezaji wa miongozo
ya kinga kwa ujumla ili uzoefu uliopatikana uendelee kwa ajili ya kudhibiti
magonjwa yote ya kuambukiza na kuipungizia Serikali mzigo wa kuhudumia wagonjwa
ambao wangeepuka kuugua magonjwa hayo iwapo wangepata elimu ya kujikinga na
kutekeleza kwa vitendo mfano kunawa mikono.
“tusiache kuendeleza hizi mbinu za usafi
zinazolenga kujikinga na magonjwa ya kuambukiza hususan kunawa mikono ili
tudhibiti na kutokomeza kabisa magonjwa hayo yakiwemo kipindupindu na magonjwa
yote ya tumbo yatokanayo na kula vyakula kupitia mikono isiyo safi” amesisitiza
Dkt. Gwajima.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam,
Dkt.Rashid Mfaume amesema kuwa yeye kwa kushirikiana na watendaji wenzake ndani
ya mkoa wa Dar es salaam ndani ya siku saba watakuwa wametekeleza agizo la
kuhakikisha kunakuwa na mfumo na utaratibu wa kupokea na kushughulikia kero za
wateja kwenye vituo vya huduma za afya kwa kutengeneza mabango makubwa yenye
ubora wa kipekee yakionesha namba za simu zilizoelekezwa ili wananchi wafahamu
na kuzitumia kwa wakati.
Huku Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mnazi
Mmoja, Dkt. Delila Moshi akiahidi kutekeleza agizo hilo haraka sana kwa
kusambaza mabango hayo kwenye maeneo yote muhimu waliko wateja huku akitumia
mfumo wa matangazo ya sauti kuwafikia wateja wengi zaidi.
Kwa upande wake Mratibu wa Huduma za Dharura
na Maafa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Christopher Mzava ametoa wito kwa wahudumu
wa afya kuendelea kushirikiana kwa karibu na wateja ili kuweka mazingira mazuri
ya kupokea mrejesho juu ya huduma wanazotoa kwa ajili ya kufanya maboresho
zaidi.
MWISHO
Comments
Post a Comment