Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa
Joyce Ndalichako amezindua Chuo cha Ufundi Stadi Nyamidaho kilichopo Wilaya ya
Kasulu Mkoani Kigoma.
Akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi,
Profesa Ndalichako amesema uanzishwaji wa Chuo hicho ni mwendelezo wa
utekelezaji wa azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga vyuo vya
ufundi stadi katika kila Wilaya Nchini ili kupeleka huduma hiyo karibu na
Wananchi na kuwapatia ujuzi vijana wa kitanzania.
Ndalichako amesema Chuo cha Nyamidaho
kimetokana na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na Taasisi ya World Vision ambapo
Serikali imekarabati majengo yaliyokuwepo na kujenga mengine mapya.
Waziri Ndalichako ameeleza kuwa jumla ya
Shilingi milioni 534 zilitolewa kwa ajili ya kazi hiyo na kwamba
zimetumika milioni 477 hadi ukamilishaji. Aidha ameridhia ombi la kiasi
kilichobaki kutumika kuanzisha ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kiume.
Ameongeza kuwa katika Mwaka 2019/20 vyuo
10 vya Halmashauri za Wilaya vimejengwa na kuanza kutoa mafunzo.
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali
Emmanuel Maganga ameishukuru Wizara ya Elimu kwa kukamilisha ujenzi wa chuo
hicho na amewataka wakazi wa kijiji cha Nyamidaho kuhakikisha vijana wao hasa
wa kike wanajiunga na chuo hicho.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya VETA, Peter Maduki
ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuimarisha Elimu ya Ufundi
nchini na kuongeza kuwa Chuo hicho kipya kina wanafunzi takriban 70.
Aidha ameagiza Uongozi wa VETA kutoa bure mafunzo ya kozi ya uwashi kwa
wanafunzi wanaotoka Nyamidaho.
Comments
Post a Comment