NDALICHAKO AZINDUA VETA NYAMIDAHO KIGOMA




Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezindua Chuo cha Ufundi Stadi Nyamidaho kilichopo Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma.

Akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi, Profesa Ndalichako amesema uanzishwaji wa Chuo hicho ni mwendelezo wa utekelezaji wa azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga vyuo vya  ufundi stadi katika kila Wilaya Nchini ili kupeleka huduma hiyo karibu na Wananchi na kuwapatia ujuzi vijana wa kitanzania.

Ndalichako amesema Chuo cha Nyamidaho kimetokana na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na Taasisi ya World Vision ambapo Serikali imekarabati majengo yaliyokuwepo na kujenga mengine mapya.

Waziri Ndalichako ameeleza kuwa jumla ya Shilingi milioni 534 zilitolewa  kwa ajili ya  kazi hiyo na kwamba zimetumika milioni  477 hadi ukamilishaji. Aidha ameridhia ombi la kiasi kilichobaki kutumika kuanzisha ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kiume.

Ameongeza kuwa katika Mwaka 2019/20  vyuo 10 vya Halmashauri za  Wilaya vimejengwa na kuanza kutoa mafunzo.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali Emmanuel Maganga ameishukuru Wizara ya Elimu kwa kukamilisha ujenzi wa chuo hicho na amewataka wakazi wa kijiji cha Nyamidaho kuhakikisha vijana wao hasa wa kike wanajiunga na chuo hicho.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya VETA, Peter Maduki ameishukuru Serikali  kwa kuendelea kuimarisha Elimu ya Ufundi nchini  na kuongeza kuwa Chuo hicho kipya kina wanafunzi takriban 70. Aidha ameagiza Uongozi wa VETA kutoa bure mafunzo ya kozi ya uwashi kwa wanafunzi wanaotoka Nyamidaho.


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.