Na. Mwandishi Wetu, MOROGORO
Shilingi bilioni 175.6 kutatua
changamoto ya maji mjini Morogoro ikiwa ni moja ya hatua za Serikali ya
Awamu ya Tano kuwapatia wananchi huduma bora za maji safi na salama katika
maeneo yote.
Akizungumza leo June 27, 2020 jijini Dodoma wakati wa kutiliana saini
mkataba wa mkopo wa masharti nafuu kutoka Shirika la Maendeleo la Ufaransa
(AFD) Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Doto James amesema kuwa utekelezaji wa
mradi huu utawezesha wakazi wapatao 722,000 kupata maji safi na salama katika
mji huo.
“Kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda
kutoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Ufaransa
kupitia AFD kwa ushirikiano mzuri uliopo unaowezesha kutekelezwa kwa miradi
mingi ya maendeleo kwa mikopo ya masharti nafuu”, alisisitiza Bw. James.
Akifafanua amesema kuwa upatikanaji wa maji utaongezeka katika mji
wa Morogoro kutoka mita za ujazo 33,000 kwa siku hadi kufikia mita za ujazo 89,
000 kwa siku baada ya kukamilika kwa mradi.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya
Maji, Prof. Kitila Mkumbo amesema kuwa utekelezaji wa mradi huo katika mji wa
Morogoro utatatua changamoto ya maji kwa wakazi wake na kuchochea maendeleo.
“Miradi ya maji 1423 inatekelezwa kote nchini huku 792
imekamika na inatoa huduma kwa wananchi ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi
ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli ambapo
mwaka 2015 aliahidi kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji vijijini na
mijini”, alisisitiza Prof. Mkumbo.
Akifafanua amesema kuwa utekelezaji wa mradi huo utoa fursa za
ajira kwa watanzania na viwanda vya ndani vitaweza kunufaika kwa
kuzalisha mabomba na vifaa vingine vinavyohitajika katika mradi huo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la Ufaransa
hapa nchini, Bi. Stephanie Mouen Essombe amesema kuwa Shirika hilo litaendelea
kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kutekeleza miradi ya maendeleo.
Akifafanua amesema kuwa mradi huo utawezesha wakazi wa Manispaa ya
Morogoro kufikiwa na huduma ya maji safi na salama kwa asilimia 90 ifikapo
mwaka 2025.
AFD imeshatoa bilioni 655 katika kipindi cha miaka 10 katika sekta
ya maji hapa nchini na hivyo kuchochea maendeleo.
MWISHO
Comments
Post a Comment