Na. Revocatus Kassimba, MOROGORO
Wizara ya Kilimo imekubaliana na Chuo Kikuu cha
Kilimo Sokoine kuanza kuzalisha mbegu bora za mazao ya kilimo ili kujitosheleza
na mahitaji ya wakulima nchini.
Makubaliano hayo yamebainishwa hivi karibuni na
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya alipokutana kwa mazungumzo na
Menejimenti ya Chuo hicho mjini Morogoro na kueleza kuwa nchi bado
haijajitosheleza na mbegu bora.
“Tunahitaji ushirikiano wa kuzalisha mbegu bora za
mazao ya kilimo kwa wingi ndani ya nchi ili kukidhi mahitaji ya wakulima”
alisisitiza Katibu Mkuu.
Wizara ya Kilimo inapenda chuo Kikuu cha Sokoine kianzishe
vitalu vya uzalishaji mbegu bora za mazao ya mboga mboga na matunda ili
kupunguza utegemezi toka nje ya nchi.
“Ifike hatua nchi yetu kuwa na uhakika wa mbegu
bora na hai. Hii itaongeza ajira kwa vijana na wakulima kupata manufaa” alisema
Katibu Mkuu Kusaya.
Kusaya alitaja maeneo mengine ya ushirikiano na
Chuo Kikuu cha Sokoine kuwa ni kuanzisha maabara bora ya kilimo ili kusaidia
mapinduzi katika utafiti, uanzishwaji wa mashamba darasa kwa wahitimu wa masomo
ya kilimo na kujenga maabara ya kisasa ya kupima ubora wa mazao yakiwemo mboga
mboga na matunda kabla ya kusafirisha nje ya nchi ili kuongeza thamani ya
bidhaa za kilimo.
Pia uhamasishaji matumizi ya teknolojia ya bora ya
uzalishaji kwa kutumia zana za kisasa na utoaji huduma za ugani na mafunzo ya
muda mfupi kwa wataalam wa wizara na wakulima kwa kutumia vyombo vya habari na
TEHAMA.
Ili kuwa na kilimo chenye tija na manufaa kwa
mkulima, Katibu Mkuu Kusaya amekiomba chuo cha Sokoine kusaidia jitihada za
wizara kudhibiti visumbufu vya mimea na mazao kama viwavijeshi, ndege
waharibifu wa kwerea kwerea, nzige wa jangwani, panya na magugu yanayoathiri
mazao ya wakulima.
Wakurugenzi wa Idara toka wizara ya Kilimo wakiwa kwenye kikao na Menejimeti ya Chuo Kikuu cha Sokoine na kujadili ushirikiano wa kuongeza tija na uzalishaji mazao nchini |
“Tunahitaji sifa nzuri ya ubora wa mafunzo na
wataalam wa chuo kikuu cha Sokoine iendelee
na kuwanufaisha wakulima kuongeza tija na uzalishaji kwa kudhibiti visumbufu vya mazao yake”.
alisema Kusaya.
Kwa mujibu wa takwimu za wizara ya kilimo kuwa
uzalishaji wa ndani wa mbegu bora umefikia tani 61,703 mwaka 2019.
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha
Kilimo Sokoine Prof. Raphael Chibunda alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa
kutembelea chuo hicho na kuwa wapo tayari kuanzisha mafunzo maalum ya muda
mfupi kwa ajili ya kufundisha wataalam waliopo kazini na wale wanaopenda
kujifunza kilimo cha kisasa.
Prof. Chibunda alisema SUA itaendeleza ushirikiano
na Wizara ya Kilimo kupitia taasisi za utafiti wa Kilimo (TARI) na kampuni ya
mbegu nchini (ASA) na Taasisi ya Udhibiti wa Mbegu Tanzaia (TOSCI) kuzalisha mbegu
bora za mazao kwa kutumia teknolojia na wataalam waliopo nchini.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya (katikati) akiongozana na Makamu Mkuu wa Chuo cha Sokoine, Prof. Raphael Chibunda (kulia) kukagua miradi ya chuo hicho leo mjini Morogoro |
“SUA ina msitu wa wataalam hivyo tunaahidi
tutashirikiana na wizara ya kilimo kufanya tafiti za mbegu bora na pia
kuzalisha mbegu hizo kwa matumizi ya ndani na nje ya nchi” alisitiza Prof. Chibunda.
Aliongeza kusema kina mkakati wa kuanzisha digrii
maalum itakayosaidia kuzalisha wataalam wabobezi kwenye usimamizi wa sekta ya
ushirika na kilimo nchini ili kuunga mkono jitahada za serikali kuwa na
ushirika imara.
Katika hatua nyingine Prof. Chibunda aliomba
Serikali iweke utaratibu wa kuratibu waduka ya pembejeo ili yawe na wataalam
waliosomea kilimo na mifugo kwa ajili ya kutoa huduma za ushauri kwa wakulima.
Katibu Mkuu huyo wa wizara ya Kilimo alisema lengo
la wizara yake ni kuhakikisha kunakuwepo sera nzuri na mazingira wezeshi ya
kufanya kilimo kuwa ajira, uchumi na biashara kwa watanzania walio wengi.
Mwisho
Comments
Post a Comment