Na. Revocatus Kassimba, MOROGORO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya
ametoa onyo kali kwa wakandarasi waliozembea kukamilisha miradi ya ujenzi wa
miundombinu ya skimu za umwagiliaji wilaya ya Mvomero na Kilosa.
Kusaya ametoa onyo hilo hivi karibuni wakati
alipoongoza ziara ya wajumbe wa kamati ya tendaji ya utekelezaji wa Mradi wa
Kuongeza thamani zao la mpunga (Extending Rice Production Project-ERPP) katika
mkoa wa Morogoro.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Kusaya (aliyeshika kofia) akiwa
na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira ,Balozi Joseph Sokoine
wakikagua mradi wa ujenzi ghala la kuhifadhia mpunga kijiji cha Kigugu wilaya
ya Mvomero
Makatibu Wakuu wengine walioshiriki ziara hiyo ni
Prof.Riziki Shemdoe (Viwanda na Biashara) pia Naibu Katibu Mkuu Balozi Joseph
Sokoine (Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira) na Naibu Katibu Mkuu Gerald Mweli
(Ofisi ya Rais-Tamisemi).
“Hatujaridhishwa kabisa na wakandarasi wa ujenzi
wa maghala ya kuhifadhia nafaka ya kijiji cha MbogomKomtonga na Kigugu kwa
kutokamilisha kazi ndani ya mkataba” alisema Kusaya kwa niaba ya kamati hiyo.
Katika hali isiyo ya kawaida kamati ya Makatibu
Wakuu ilichukizwa na kitendo cha mkandarasi M/s AMI & VAI Investment ya Dar
es Salaam anayejenga ghala la kuhifadhia mpunga kijiji cha Kigugu wilaya ya
Mvomelo kwa gharama ya shilingi Milioni 816.37 alikimbia eneo
la mradi licha ya kuwa na taarifa za ujio wa makatibu wakuu.
Alipoulizwa alipo mkandarasi wa mradi
huo,msimamizi wa mafundi Abdul Kabanika alisema
“ Bosi tulikuwa naye hapa muda mfupi uliopita lakini sasa hatumuoni”.
Taarifa zilisema kampuni hiyo ya M/s Ami & Vai
Investment imeshindwa kumaliza kazi ndani ya mkataba ulioisha tarehe 21 Aprili
2020 na ujenzi upo asilimia 70.
“Natoa muda hadi ifikiapo saa 11 jioni leo
(Jumatano) mkandarasi M/s AMI & VAI Investment awe amejisalimisha
kwangu,kwani ajue serikali ina mkono mrefu. Tutamsaka kotote na kumrejesha hapa
Kigugu atueleze kwanini kazi yetu hajakamilisha” alisema Kusaya.
Kamati ilikagua pia mradi wa ghala kijiji cha
Mbogo Komtongo ambao ujenzi wake umefikia asilimia 70 chini ya mkandarasi M/s
Shekemu kwa gharama ya Shilingi Milioni 790.87 lakini haujakamilika.
Katibu Mkuu Kusaya alionya na kusema kutokamilika
kwa miradi hii kutakua ni kikwazo kwa wakulima kukosa mahala pa kuhifadhi mazao
yao na lengo la serikali kutotimia.
Awali kamati hiyo ilitembelea skimu ya umwagiliaji
kijiji cha Mvumi wilaya ya Kilosa na kujionea hali ya miundombinu kwa ajili ya
mashamba ya mpunga ya wakulima iliyofikia asilimia 84 ya ujenzi mitaro na
banio.
Skimu hiyo inajengwa kwa gharama ya shilingi
Bilioni 1.97 na mkandarasi M/s Whitecity International Ltd akishirikiana na M/s
Skyline Properties Ltd na kwa mujibu wa mratibu wa mradi kiasi cha shilingi
Milioni 713.15 zimelipwa sawa na asilimia 54.
Alipoulizwa kwanini mradi haujakamilika msimamizi
wa mradi huo, Mhandisi Emanuel Norbet alisema wamechelewa kukamilisha kutokana
na uwepo wa mvua nyingi msimu huu zilizoharibu miundombinu ya barabara na
mitaro.
Katika hatua nyingine, kamati iliridhishwa na
kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa ghala la kuhifadhia mazao kijiji cha Mvumi
wilaya ya Kilosa kwa asilimia 99 lililojengwa na mkandarasi M/s B.H Ladwa Ltd
kwa gharama ya shilingi milioni 971.31 ambapo tayari shilingi milioni 536.06
zimelipwa.
Baada ya ukaguzi wa miradi hiyo Katibu Mkuu Wizara
ya Kilimo alisema serikali itahakikisha sheria inachukuliwa ili mkradi
ikamilike kwa mujibu wa mikataba.
“Mikataba yote
imekwisha, nataka miradi hii iishe na wakulima wapate maji kwa ajili ya
kutekeleza kalenda zao za kilimo na serikali ya Rais John Magufuli haitaki
wakandarasi wazembe. Tunataka wakulima wapate maji kwenye mitaro ili waendelee
na kilimo cha mpunga” alisema Kusaya.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na
Biashara Prof.Riziki Shemdoe amewaagiza washauri wasimamizi wa miradi hiyo
ambayo haijakamilika kuchukua sheria na kuanza kukata fedha kwa wakandarasi
wazembe.
“Hatua za kisheria kukata fedha kwa mujibu wa mkataba
zichukuliwe haraka,kwani mikataba imeisha na muda wa nyongeza umeisha. Fedha ya
serikali ianze kukatwa kila siku (liqudated damages)“ alisema Prof. Shemdoe.
Akizungumza hatua alizochukua msimamizi wa miradi ya
ujenzi wa maghala Kigugu na Mbogo Komtonga, Architect Ismail Mvungi aliwajuisha
wajumbe kuwa tayari wameanza kuwakata wakandarasi hao kiasi cha shilingi 400,00
kila siku kwa kuchelewa kukamilisha kazi.
Mradi wa mradi wa ERPP, Mhandisi January Kayumbe
alisema miradi hiyo ya ujenzi ilitekelezwa kwa mwaka mmoja na muda wake
unamalizika 30 Aprili 21 mwaka huu, hivyo wakandarasi ambao hawajakamilisha
taratibu za sheria zitafuatwa.
Akishukuru kwa niaba ya wananchi Mwenyekiti wa
Kijiji cha Kigugu kata ya Sungija wilaya ya Mvomelo, Damas Mnyani alisema miradi
hii itasaidia kuongeza uhakika wa upatikanaji maji kwenye mashamba ya mpunga
hali itakayoongeza uhakika wa uzalishaji.
“Kuwepo kwa skimu hizi kwenye vijiji vyetu
kutasaidia kuondoa tishio la njaa kwani tutalima mpunga mwaka mzima na
kuhifadhi kwenye maghala tuliyojengewa na serikali yetu.” Mnyani.
Mradi huo umefanikiwa hadi sasa kuongeza
uzalishaji zao la mpunga toka tani 2.5 kwa ekari hadi tani 5.5 kwa ekari baada
ya miundombinu kuboreshwa.
Mradi wa ERPP ulianza kutekelezwa mwaka mwaka 2015
kwa gharama ya Dola za kimarekani milioni 22.91 toka Benki ya Dunia ukijusisha
Tanzania Bara na Zanzibar.
Jumla ya
miradi 11 ikiwemo ujenzi wa skimu 5 za umwagiliaji,ujenzi wa maghala 5 na
ujenzi wa maabara moja ya mbegu inatekelezwa
katika mkoa wa Morogoro chini ya ERPP.
Mwisho
Comments
Post a Comment