DAR
ES SALAAM.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul
Makonda ametoa msaada wa Mabati yenye Thamani ya shilingi Milioni 476 kwaajili
ya Kuezeka Nyumba 1,000 za Wajane mkoani humo ambao nyumba zao zimeathiriwa na
mafuriko yanayotokana na Mvua zinazoendelea kunyesha ambapo amewataka Wananchi
waliojenga mabondeni kuondoka.
RC Makonda amesema hayo wakati wa Ziara ya
Kukagua athari za Mvua na kubaini uwepo wa familia za Wajane ambao Nyumba
zao zimechukuliwa na Mafuriko na sasa wanapitia changamoto ya kuhifadhiwa kwa
majirani baada ya kukosa makazi ya kuishi hivyo ameona ni busara kutoa msaada
huo kama sehemu ya pole kwa adha waliyoipata.
Aidha RC Makonda amewapa siku 10 Wakuu wa
Wilaya kuhakikisha wanapitia maeneo ya Mito na Mabonde kukagua athari za
mabadiliko ya tabia nchi kwa kuwashirikisha viongozi wa mitaa ili kwa pamoja
watoe mapendekezo ya nini kifanyike kisha wampatie ripoti ya kuonyesha hatua za
kukabiliana na Mafuriko ya Mara kwa Mara.
Aidha RC Makonda amesema athari zinazoonekana
kwa sasa ni matokeo ya Jamii kuwafumbia macho watu wanovunja sheria kwa kujenga
mabondeni, kuchimba mchanga na kuziba mikondo ya maji jambo linalopelekea
Mafuriko hivyo ametaka kila mwananchi kuwa mlinzi wa mwenzake.
Pamoja na hayo RC Makonda amesema kwa sasa serikali
inaendelea kurejesha miundombinu na madaraja yaliyochukuliwa na Mafuriko
ikiwemo ujenzi wa madaraja ya muda mfupi ili kuwezesha shughuli za kijamii
kuendelea.
RC Makonda pia amewaelekeza wakandarasi
kutumia kipindi hiki cha mvua kuangalia kama Design ya madaraja wanayojenga
yanakidhi kuhimili na kupitisha maji ya mvua ili wabuni design mpya zinazokidhi
viwango.
Comments
Post a Comment