Na. Revocatus Kassimba, MOROGORO
Vijana wahitimu wa vyuo mbalimbali nchini
wameshauriwa kujitokeza na kupata mafunzo kwa vitendo kuhusu kilimo biashara
kwa ajili ya kujipatia ujuzi na ajira toka Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine.
Wito huo umetolewa jana na Katibu Mkuu Wizara ya
Kilimo, Gerald Kusaya wakati akiongea na vijana wanaondelea na mafunzo kwa
vitendo kuhusu kilimo biashara katika Kituo Atamizi cha Vijana cha Kilimobiashara
(SUA-AIC Youth Agribusiness Incubators) mjini Morogoro.
“Vijana tunatambua uwepo wenu hapa
kituoni,jitahidini kujifunza mbinu bora za kilimo mkilenga kujiajili na mwisho wa mafunzo yenu mrudi vijijini na
mijini kuwa walimu kwa vijana wenzenu” alisema Kusaya.
Katibu Mkuu Kusaya aliwapongeza vijana hao kwa
kuamua kujiunga na kambi atamizi kwani wanatekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya
Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuwataka vijana kujiajili kupitia kilimo.
“Lengo la serikali ya Awamu ya Tano ni kukifanya
kilimo kuwa ni ajira na kazi inayochangia kukuza uchumi wa nchi,ndio maana nimekuja
kuwatembelea na kuwatia moyo “ alisisitiza Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo.
Akitoa taarifa ya kituo hicho,Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Kilimo Sokoine, Prof. Raphael Chibunda alisema kituo atamizi
kinafundisha vijana wahitimu wa vyuo mbalimbali wanaopenda kufanya kilimo
biashara.
Alisema kwa sasa kuna vijana wapatao 40
wanaoendelea na mafunzo kwa vitendo kwa mwaka mmoja wakizalisha mazao ya mboga
mboga kama hoho za rangi,matango na nyanya kwa usimamizi wa wataalam wa chuo.
Akielezea manufaa ya kituo hicho Hefsiba Olloo
kutoka Kilimanjaro alisema ameweza kuzalisha nyanya kwenye kitalu nyumba na
kuvuna kilo 1,318 za nyanya zilizompatia shilingi milioni 4 ndani ya kipindi
cha miezi minne.
Mafanikio aliyopata mwaka huu Januari alivuna kilo
(338) Februari (400),Machi (400) na Aprili amevuna (180) ambazo ameuza kwa bei
ya shilingi 2500 hadi 3000 kwa kilo moja.
“Kwa muda
mfupi tangu nimejiunga na kambi atamizi hapa SUA mwezi Septemba 2019 tayari
nimeona manufaa yake kwa kuwa na uhakika wa kipato kupitia kilimo cha nyanya
.Nilipanda nyanya mwezi Octoba mwaka 2019 na sasa naendelea kuvuna” alisema
Hefsida.
Hefsida alihitimu shahada ya Sayansi katika Hisabati (Bachelor of Science in
Mathematics) Chuo Kikuu cha Dodoma mwaka 2018 na hakuweza kupata ajira hivyo
akaamua kuanzisha kilimo cha mboga.
Kwa upande wake msimamizi wa kituo atamizi Zebedayo
Sanga ambaye ni mhitimu wa digrii ya Horticulture mwaka 2018 toka SUA
aliwahamasisha vijana wengi zaidi waliopo mitaani kuja kujifunza kilimobiashara
na kuwa na uhakika wa kipato na ajira.
Mwisho
Comments
Post a Comment