SIMAMIENI MIRADI KWA KUZINGATIA MATUMIZI YA VIFAA KATIKA VIWANGO VILIVYOELEKEZWA NA SERIKALI-MWAMBAMBALE



Na Mwandishi wetu,  Kilosa

Wito umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa Asajile Mwambambale kwa wasimamizi mbalimbali wa miradi na kamati za ujenzi katika kata na vijiji kuhakikisha shughuli zote za ujenzi zinazingatia maelekezo ya viwango vya vifaa vilivyoelekezwa na Serikali. 

Mwambambale ametoa maelekezo hayo wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa miradi akiwa ameambatana na timu ya menejimenti ya Halmashauri ambapo amesema kuwa vifaa hivyo vinapaswa kukidhi mahitaji na viwango vilivyoelekezwa na Serikali ili kupata matokeo mazuri  ya miradi hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kutumika na vizazi vijavyo.

Akiwa ameambatana na timu ya menejimenti katika kituo cha afya Malolo  ameelekeza kuwa wakati wa kiangazi nguvu kazi ya wananchi ianze kuandaa matofari kwa ajili ya wodi tatu kwa maana ya wodi ya wanaume, wanawake na watoto sambamba na jengo la kuhifadhia maiti, huku akisema kuwa ni matumaini yake kuwa kituo cha Malolo kitakapokamilika kitatoa huduma zote za msingi ili kuwaondolea wananchi adha ya kwenda umbali mrefu kupata huduma huku akisema kituo hicho kitahudumia wananchi wengi toka maeneo mbalimbali.

Aidha amesema kuwa anatarajia kuanzia mwezi Julai kituo hicho kitakuwa kimefanya maandalizi  ya kutosha na kwamba ofisi ya Mkurugenzi inategemea kuanza kupokea mahitaji ya uwezeshwaji wa vifaa na ufundi kwa ajili ya wodi hizo na kwamba kama Wilaya ingependa ujenzi katika kituo hicho kukamilika kwa wakati ili huduma zianze kutolewa mara moja kwa wananchi ambapo kituo hicho kinatarajiwa kukamilika mwezi Mei na kwamba kituo cha afya Malolo ni kituo cha mfano kwani kimejengwa na wananchi wenyewe.

Akijibu changamoto zilitolewa za uhaba wa watumishi wa idara ya elimu na kilimo Mkurugenzi amesema litafanyiwa kazi huku akiitaka idara ya Kilimo kufanyia kazi changamoto ya ugonjwa wa zao la vitunguu,  sambamba na hayo ameahidi kuchimbwa kwa kisima kirefu katika kata ya Malolo kazi itakayofanywa na Halmashauri ili kutatua changamoto ya uhaba wa maji ambayo wananchi wamekuwa wakitumia maji ya mtoni ambayo yamekuwa yakisababisha ugonjwa wa kichocho.

Kwa upande wa kituo cha afya Mikumi ambacho ujenzi wa wodi mbili za wanawake na wanaume unaendelea amesema kwa siku za baadaye kinatarajiwa kiweze kupata hadhi ya kuwa  sawa na hospitali ili kiweze kuhudmuia wanacnhi wengi kwa kadri inavyowezekana kwani huduma za mahali hapo zinalenga zaidi kuhudumia wananchi kwa bei nafuu lakini pia ametaka ujenzi wa wodi hizo kasi iongezwe ili ifikapo mwezi Aprili wodi hizo ziwe zimekamilika ambapo ujenzi huo unafadhiliwa na fedha za Serikali una unatarajiwa kutumia shilingi milioni 140 na kwasasa uko katika hatua za upauaji.


Nao wananchi wa kata za Malolo na Mikumi wameshukuru kwa ujenzi unaondelea katika maeneo yao kwani kabla ya kuwepo kwa vituo hivyo walikuwa katika adha kubwa ya kutafuta huduma katika maeneo ya jirani ambapo walikuwa wakitumia gharama kubwa ili kupata huduma lakini pia kutembea umbali mrefu jambo linalowagharimu fedha na muda lakini kwa sasa wanashukuru kwani adha hizo zimeanza kutoweka na kwamba wanatarajia huduma zote za msingi zitakapotolewa katika vituo hivyo zitakuwa zimewapunguzia gharama mbalimbali kama za matibabu na usafiri.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.