Na Munir Shemweta, WANMM MUSOMA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline
Mabula amesema wizara yake itaipatia ofisi ya ardhi mkoa wa Mara vifaa vya
upimaji ili viweze kutumiwa na halmashauri za mkoa huo kwa lengo la
kuongeza kasi ya upimaji.
Dkt Mabula alitoa kauli hiyo jana wilayani Musoma mkoa wa Mara
alipokwenda kukagua ofisi mpya ya ardhi ya mkoa Mara ikiwa ni jitihada za
wizara ya ardhi kusogeza huduma za ardhi kwa wananchi.
Awali huduma za ardhi zilikuwa zikitolewa na ofisi za Mkamishna
Wasaidizi wa Kanda ambapo kanda moja ilikuwa ikihudumia zaidi ya mikoa miwili
jambo lililokuwa likiwapa usumbufu wamiliki wa ardhi kwenda umbali mrefu
kuifuata huduma hiyo.
Alisema, baada ya wizara yake kuanzisha ofisi za mikao sasa
wananchi watapata huduma za ardhi katika mikoa husika na migogoro ya ardhi sasa
itapatiwa ufumbuzi kupitia wataalamu watakaokuwa katika mikoa hiyo.
Alibainisha kuwa, katika jitihada za kuongeza kasi ya upimaji
maeneo mbalimbali ofisi za mikoa zitapatiwa vifaa vya upimaji ili visaidie
halmashauri kupanga, kupima na kumilikisha ardhi na kusisitiza vifaa hivyo
vitatolewa bure na aliwataka wakurugenzi wa halmashauri kushirikiana na ofisi
za ardhi za mikoa.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri Mabula, Wizara yake imeamua kubeba
jukumu la kutoa vifaa vya upimaji ili kuongeza kasi ya upimaji ingawa jukumu
hilio linapaswa kufanywa na halmashauri kwa kuwa ndizo zenye mamlaka za
upangaji miji katika maeneo.
Dkt Mabula amesikitishwa na kiasi kidogo kinachotengwa na
halmashauri kwa ajili ya kazi za kupanga, kupima na kumilikisha ardhi ambapo
alitolea mfano wa halmasahauri ya Musoma kutenga milioni 30 kwa kazi mbalimbali
za sekta ya kiasi alichokieleza kuwa kidogo.
‘’Milioni 10 au 15 utapima viwanja vingapi? Halmashauri
hazijaipa kipaumbele sekta ya ardhi ndiyo maana malalamiko yanakuwa mengi,
muongeze bajeti za upimaji’’ alisema Dkt Mabula
Hata hivyo, ameishauri halmashauri ya wilaya ya Musoma kuwatumia
wataalamu wake kwa kuandika andiko ili kupatiwa mkopo usio na riba unaotokewa
na wizara kwa ajili ya shughuli za umilikishaji ardhi ambapo alisema katika
kipindi caha bajeti ijayo wizara inatarajia kupata bilioni saba kwa ajili ya
kuzikopesha almashauri.
Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Musoma Dkt Vincent Naano Anney
aliipongeza wizara ya ardhi nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa uamuzi wake wa
kuanzisha ofisi za mikoa na kueleza kuwa uamuzi huo utaleta nafuu
kwa wananchi wa mara katika kupata huduma za ardjhi ambapo awali iliwalazimu
kusagiri hadi Simuiyu kupata huduma hiyo.
Comments
Post a Comment