Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo
ya Makazi, Dkt. Angeline Mabula amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC)
kukamilisha haraka mradi wake wa ujenzi wa Jengo la Kitega Uchumi lililopo
mpaka wa Tanzania na Uganda eneo la Mutukula wilaya ya Misenyi mkoani Kagera
ili kuliwezesha shirika kupata faida kupitia jengo hilo.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angelina Mabula (Kulia) |
Dkt. Mabula alitoa agizo hilo juzi wakati
akikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo akiwa katika ziara yake mkoani
Kagera kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo sambamba na kufuatilia utekelezaji
maagizo aliyoyatoa kuhusiana na wa sekta ya ardhi.
Alisema, mradi wa jengo la kitega uchumi
unaoendelea eneo la Mutukula uko sehemu nzuri ya mpakani mwa Tanzania na Uganda
na kuna muingiliano mkubwa wa kibiashara hivyo ni vizuri Shirika la Nyumba
likaona haja ya kuharakisha ujenzi wake ili kutoa fursa kwa taasisi na
wawekezaji kupanga kwenye jengo hilo.
Kwa mujibu wa Dkt. Mabula, mji wa
Mutukula umechangamka na una mzunguko mzuri wa biashara hatua inayosababisha
kuwepo mvuto kwa wafanyabiashara na wawekezaji katika eneo hilo na kukamilika
kwake kutaiwezesha NHC kupata wapangaji na kujipatia mapato.
“Naagiza Miradi yote ya Shirika la Nyumba
la Taifa inayoweza kuliingizia Shirika mapato likiwemo hili la kimkakati lazima
iishe ili NHC iingize mapato na kujiendesha kibiashara’’ alisema Dkt. Mabula .
Kwa upande wake Meneja wa Shirika la
Nyumba la Taifa (NHC) mikoa ya Kagera na Geita, Benit Masika alisema shirika
lake liko katika jitihada kubwa za kuhakikisha mradi huo wa jengo la kitega
uchumi Mtukula unakamilika mapema na kubainisha kuwa kwa sasa ujenzi wake
umefikia asilimia 88 na utakapokamilika litapangishwa kwa taasisi zilizoonesha
nia ya kupanga zikiwemo za kifedha kama vile mabenki.
Aidha, Nabu Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi aliitaka Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi mkoani Kagera
kutumia vizuri fursa ya kuwa eneo la mpakani kwa kuhakikisha inakamilisha zoezi
la kupanga, kupima na kumilikisha viwanja ili wananchi waweze kujenga nyumba
nzuri na zenye sura ya nchi ya Tanzania.
Alisema, Halmashauri ya Misenyi wakati wa
kupanga mji huo ihakikishe inakuwa na soko la mazao zikiwemo ndizi ili
kuwawezesha watanzania kuuza bidhaa zao nchini Uganda tofauti na sasa ambapo
tegemeo kubwa lipo upande wa Uganda na kuwataka watanzania kubadilika kwa
kuitumia fursa ya kuwa eneo la mpakani kuchangamkia kuwekeza katika ardhi.
MWISHO
Comments
Post a Comment