Na Munir Shemweta, WANMM, MUSOMA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline
Mabula ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa
Mara iliyoko Kwangwa Musoma unaogharimu takriban Bilioni 15.082.
Dkt Mabula aliridhishwa na kasi ya mradi wa ujenzi wa hospitali
hiyo alipokwenda kukagua maendeleo ya ujezi wake jana wakati akiwa katika ziara
ya siku moja mkoani Mara.
Alisema, ujenzi wa mradi huo ni ukombozi kwa wananchi wa Mara
sambamba na mikoa na nchi jirani kwa kuwa itakuwa ikitoa huduma za kitabibu kwa
wananchi wa maeneo hayo.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi alibainisha
kuwa, hana mashaka na Shirika la Nyumba la Taifa katika kutekeleza mradi huo
kutokana na Shirika hilo kufanya vizuri kwenye miradi mbalimbali inayosimamia.
‘’Kwa sasa sina mashaka na Shirika la Nyumba la Taifa katika
masuala ya ujenzi kutokana na kufanya vizuri kwenye miradi mingi ya ujenzi
inayosimamia lakini kinachotakiwa hapa ni kukamilisha ujenzi kwa wakati’’
alisema Dkt Mabula
Ameitaja baadhi ya miradi ya ujenzi inayofanywa na NHC na
kufanya vizuri kwenye maeneo mablimbali kuwa ni ujenzi wa ofisi kumi na saba za
Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Hospitali ya Rufaa ya
Kusini iliyopo Mtwara, Ofisi ya wilaya ya Wang’ingombe na nyumba za wakuu wa
wilaya za Hai na Ulanga.
Kwa upande wake Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa
Mara Goodluck Thomas alisema Shirika lake katika kutekeleza mradi huo tayari
baadhi ya kazi zimekamilishwa ikiwemo jengo la Huduma ya Mama na Mtoto,
nyongeza ya ghorofa moja na kupaua, kupiga plaster nje na ndani, maandalizi ya
rangi, fremu za milango pamoja na kuweka marumaru.
Kwa mujibu wa Goodluck, kazi zinazoendelea sasa ni uwekaji
mifumo ya maji safi na maji taka, kazi ya umeme, uwekaji mifumo ya gesi,
ufungaji madirisha ya alminiuam na ukamilishaji kazi nyingine ukiendelea na
mradi wa ujenzi wa hospitali hiyo umefikia asilimia 65.
Mkuu wa wilaya ya Musoma Dkt Vincent Naano Anney alimueleza
Naibu Waziri wa Ardhi kuwa wakati ujenzi wa hospitali hiyo ukiendelea
kukamilishwa kuna haja kwa mamlaka husika kuanza kuangalia mahitaji
ya Wataalamu na Vifaa vinavyohitajika kwenye vitengo mbalimbali vya hospitali
hiyo na kubainisha kuwa kazi hiyo isipofanyika mapema kuna hatari ujenzi
utakapokamilika hospitali hiyo ikakosa wataalamu wa kutosha kutokana na ukubwa
wake.
Comments
Post a Comment