MKURUGENZI KILOSA DC AONGOZA CMT KUKAGUA MIRADI YA MAENDELEO


Na. Gladys Gabriel, KILOSA
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Asajile Mwambambale amewataka wasimamizi wa miradi na kamati za ujenzi katika kata na vijiji kuhakikisha shughuli zote za ujenzi zinazingatia viwango na vya vifaa vinavyotumika katika ujenzi ni vile vilivyoelekezwa na Serikali.

Maelekezo hayo ameyatoa leo katika ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa.

Mkurugenzi Mwambambale amesema kuwa vifaa vinavyotumika katika ujenzi vinapaswa kukidhi mahitaji na viwango vilivyoelekezwa na Serikali ili kupata matokeo mazuri ya miradi hiyo. Kufuata maelekezo hayo kutaifanya miradi inayojengwa kudumu kwa muda mrefu na kutumika na vizazi vijavyo, aliongeza.

Katika Kituo cha Afya Malolo, Mkurugenzi huyo ameelekeza kuwa wakati wa kiangazi nguvu kazi ya wananchi ianze kuandaa matofari kwa ajili ya wodi tatu za kituo hicho. Alizitaja wodi hizo kuwa ni wodi ya wanaume, wodi ya wanawake na watoto sambamba na jengo la kuhifadhia maiti.


Alisema kuwa kituo hicho cha Afya kitakapokamilika kitatoa huduma zote za msingi ili kuwaondolea wananchi adha ya kusafiri umbali mrefu kupata huduma za afya wilayani humo. Kituo hicho kitahudumia kitahudumia wananchi wengi toka maeneo mbalimbali ya Halmashauri hiyo, alisisitiza.

Aidha, amesema kuwa anatarajia kuanzia mwezi Julai kituo hicho kitakuwa kimefanya maandalizi ya kutosha na ofisi yake inategemea kuanza kupokea mahitaji ya uwezeshwaji wa vifaa na ufundi kwa ajili ya wodi hizo. Ameongeza kuwa matarajio ya Wilaya ujenzi wa kituo hicho kukamilika kwa wakati ili huduma zianze kutolewa mapema kwa wananchi. Mkurugenzi amekitaja kituo hicho kuwa cha mfano kutokana na kujengwa na wananchi wenyewe.


Katika kituo cha Afya Mikumi ambapo ujenzi wa wodi mbili za wanawake na wanaume unaendelea Mkurugenzi Mwambambale amesema kwa siku za baadaye kinatarajiwa kiweze kupata hadhi ya kuwa sawa na hospitali. Kupanda hadhi kituo hicho kutawezesha kupanua wigo wa uhoaji huduma na kiweza kuhudumia wananchi wengi kwa kadri inavyowezekana, aliongeza kwa gharama nafuu.

Wakati huohuo, ameagiza ujenzi wa wodi hizo uongezwe kasi ili ifikapo mwezi Aprili ziwe zimekamilika. Ujenzi huo unafadhiliwa na fedha za Serikali ukitarajiwa kutumia shilingi milioni 140, ukiwa katika katika hatua za upauaji.

Nao wananchi wa kata za Malolo na Mikumi wameshukuru kwa ujenzi unaoendelea katika maeneo yao kutokana na adha kubwa ya kutafuta huduma za afya katika maeneo ya mbali kwa gharama kubwa.

Katika ziara hiyo ya kutembelea miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Mkurugenzi huyo aliambatana na timu ya menejimenti ya Halmashauri hiyo (CMT).

MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.