Afa maji akivua samaki Bonde la Mpunga wilayani Bahi


Na Mwandishi Wetu ,Dodoma
MTU mmoja anayesadikiwa kuwa na umri wa miaka 30 hadi 35 amezama kwenye maji wakati akivua samaki katika eneo la bonde la Mpunga Bahi Makulu Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma mpaka sasa juhudi za kumtafuta zinaendelea.

Akithibitisha taarifa hizo Mkuu wa Wilaya ya Bahi Mwanahamisi Mukunda amewataka wananchi kuchukua tahadhari na kuacha kufanya shughuli zao kwenye maeneo hatarishi.

“Ni kweli tukio hilo limetokea ni jambo la kusikitisha sana, tumeshawaelekeza  wananchi mabonde mengi yamejaa maji ni hatari kwa maisha yao,” alisema

Pia aliwataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhali kuifuatia mvua zinazoendelea kunyesha.

Alisema mito mingi imekuwa ikiishia katika wilaya ya Bahi hali ambayo inasababisha maji kuingia kwenye makazi ya watu na kwenye mashamba.

Aidha alitoa tahadhali kwa wazazi kuhakikisha watoto wao wako mahali salama kutokana na baadhi ya watoto kuonekana kwenye mito na madimbwi yaliyojaa maji wakiogolea.

Diwani wa kata ya Bahi Augustine Ndonu alisema tukio l mtu kuzama limetokea juzi, saa kumi jioni  maeneo ya mashamba mapya ambapo mtu huyu mwanaume alizama wakati akivua samaki aina ya kambale na mpaka sasa bado hajapatikana na juhudi za kumtafuta inaendelea.

Alisema taarifa ilishatolewa kituo cha polii na juhudi a kumtafuta bado zinaendelea.

Alisema tahadhali inaendelea kutolewa katika ofisi za kijiji, kuwataka watu anaokwenda kuvua samaki waende kwa makundi na si kila mmoja kwenda peke yake kwani maji ni mengi.

Alisema kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha na mvua iliyonyesha jana na juzi maji yamejaa na kufunika mashamba ya mpunga na hivyo kupelekea maeneo ya mabonde ya mpunga kuwa na maji na matope mengi jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa wananchi wanaojihusisha na uvuvi wa samaki.

Alisema mito mingi iliyopo Bahi, mto Bubu ambaozhutokea Kondoa, Mto Chikola na Sanza Manyoni  yote hupeleka maji kwenye bwawa la tope la Bahi.

“Hapa Bahi maji yamejaa sana na watu wengine walishindwa kupanda mpunga kutokana na maji kujaa sana na watu wamekuwa wakitumia fura hiyo kufanya uvuvi wa samaki jambo hilo ni hatari kwani maji na tope ni jingi,” alisema.

Aliwataka wananchi kucukua tahadhari hasa katika kipindi hiki cha mvua
Mwisho


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.