WAZAZI CHAMWINO WATAKIWA KUDHIBITI UTORO WA WANAFUNZI


Na. Mwandishi wetu, DODOMA
Naibu Meya aliyemaliza muda wake Jiji la Dodoma, Jumanne Ngede amesema kuwa wazazi na walezi wa Kata ya Chamwino jijini Dodoma wenye wanafunzi wanaosoma elimu ya msingi na sekondari ambao ni watoro hawatavumiliwa, badala yake wataburuzwa kwenye vyombo vya sheria ikiwemo mahakamani.
Ngede amesema hayo alipokuwa akizungumza na wajumbe wa kamati ya bodi ya shule ya msingi ya Chinangali kwenye kikao cha kutadhimini changamoto mbalimbali zinazokabili shule zilizopo kwenye kata hiyo ikiwemo za sekondari na msingi kuhusiana na utoro wa wanafunzi na miundombinu yake.
Ngede ambaye pia ni Diwani wa Kata hiyo amesema hayo kuwa hatua ya kuwaburuza mahakamani wazazi na walezi, ina malengo ya kuziona shule hizo zilizopo kwenye Kata hiyo zinafanya vizuri kwenye kitaaluma na watoto wanaosoma wale wa msingi na sekondari wanafanya vizuri kwenye kielimu pindi wanapohitimu elimu yao.
Alisema serikali kwa hivi sasa imewapunguzia makali na mzigo mkubwa kwa upande wa elimu hivyo  hakuna sababu kwa wazazi na walezi kuwavumbia macho watoto wao ambao wamekuwa na tabia ya utoro na wao kushindwa kutoa ushirikiano kwa walimu husika na kamati zilizochaguliwa kwenye shule zao.
“Ili tuweze kufika katika ushindani wa kufanya vizuri kitaaluma kwenye Wilaya yetu hii ya Dodoma ni vema wazazi, walezi, walimu na kamati ya bodi ya shule iliyochaguliwa wakao kitu kimoja ambacho kitakachowezesha kukomesha tabia na pia kutoa elimu kwa baadhi ya wazazi ambao watoto wao wamekuwa watoro” alisema.
Kwa upande wake Afisa elimu kata ya Chamwino Sponsa Mkusa alisema pamoja na serikali kuwapunguzia baadhi ya mahitaji ya wanayohitaji kwa wanafunzi, bado wana wajibu wa kuhakikisha wanachangia elimu hiyo ikiwemo katika eneo la chakula na mahitaji mengineyo ambayo yanayohusiana na mzazi na mlezi.
Mkusa alisema kuna baadhi ya mahitaji hayahusiani na serikali kama vile ununuzi wa madaftali,chakula na sare ya shule,hivyo ni lazima wazazi na walezi lazima muhusike katika kuhakikisha watoto hao wanasoma vizuri badala ya kusubiri serikali iwapatie.
Naye Mwenyekiti wa bodi ya shule ya msingi ya Chinangali alisema kuwa pamoja na hatua ya kuwachukulia wazazi na walezi wenye watoto ambao ni watoro,pia shule hiyo inakabiliwa na ukosefu wa madawati ikiwemo na vyumba suala ambalo limekuwa likisababisha walio wengi kukosa sehemu ya kukaa.
MWISHO


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.