NJOMBE MJI YAJIPANGA KUONDOA DARAJA SIFURI KIDATO CHA NNE


Na. Amiri Kilagalila, NJOMBE
Jitihada za makusudi zimetakiwa kuchukuliwa ili kuondoa sifuri na daraja la nne kwenye mitihani ya kidato cha nne katika shule za Halmashauri ya Mji wa Njombe licha ya Halmashauri hiyo kushika nafasi ya pili kwa ufaulu katika Mkoa wa Njombe.
Katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Mji wa Njombe baadhi ya madiwani akiwemo Abuu Mtamike wa Kata ya Mjimwema,Filoteus Mligo Diwani wa Kata ya Lugenge na Reginald  Danda toka Kata ya Iwungilo wamesema wao kama madiwani wamekuwa wakihamasisha jamii kutekeleza yale yanayowapasa katika kukuza elimu hatua ambayo inapaswa kuungwa mkono na serikali kwa kupeleka fedha za maendeleo na kununua madawati badala ya kusalia wakipongezana kwa kushika nafasi ya pili kimkoa.
Awali akitoa salaam za serikali Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Ruth Msafiri amesema Halmashauri ya Mji wa Njombe licha ya kufanya vizuri bado inapaswa kuongeza nguvu katika sekta ya elimu kwani bado kuna wanafunzi wanafeli mitihani yao.
Mwenyekiti wa kamati ya afya uchumi na elimu katika Halmashauri hiyo, Yurick Msemwa ambaye ni Diwani wa Kata ya Luponde amesema ili kupandisha kiwango cha ufaulu zaidi, mshikamano wa pamoja unahitajika kwa kila mmoja ndani ya Halmashauri hiyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Njombe, Iluminata Mwenda amesema wamelazimika kuanzisha kampeni ya kuondoa zero katika shule zote kwa kuboresha miundombinu ya elimu na mbinu za ufundishaji.
Katika matokeo ya kidato cha nne kwa mwaka 2019 Halmashauri ya Mji wa Njombe imeshika nafasi ya pili kimkoa ikiongozwa na Halmashauri ya Mji wa Makambako hatua ambayo imewafanya madiwani hao kuona ulazima wa kupambana ili kufuta zero na daraja la nne katika shule zote.

MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.