ZAIDI YA BILIONI 3.5 ZAKUSANYWA KUPITIA SEKTA YA MADINI MKOANI GEITA



Na. Tito Mselem, CHATO

Tangu kuanzishwa kwa masoko ya Madini nchini, Mkoa wa Geita umeongeza ukusanyaji wa mapato kwenye sekta ya Madini kutoka chini ya shilingi bilioni 1 kwa mwaka mpaka kufikia zaidi ya shilingi bilioni 3.5 kwa mwaka.
 
Waziri, Doto Biteko
Hayo yameelezwa na Waziri wa Madini, Doto Biteko alipokuwa akifungua soko kuu la Madini ya dhahabu Chato lililopo Buseresere Mkoani Geita na kwamba, soko hilo limefikisha idadi ya masoko 29 nchini na masoko 8 yaliyofunguliwa Mkoani Geita ambalo kwa sasa lina ofisi 10 za madalali (Brokers) wanao nunua Madini hayo.

Aidha, Waziri Biteko amewataka maafisa wa Serikali kutowasumbua wachimbaji na wafanyabiashara wa Madini pindi wanapopeleka Madini yao sokoni na mchimbaji au mfanyabiashaya yoyote wa Madini haruhusiwi kukaa na Madini nyumbani kwake bila ya kuwa na nyaraka kutoka serikalini.

“Kipindi cha nyuma serikali ilikuwa inatoa leseni kwa wafanyabiashara bila kujua wananunua wapi wala wanauza wapi ila leo wanunuzi wanajua wakanunue wapi na wakauze wapi, haya ni mafanikio makubwa sana kwenye sekta ya Madini na anae stahili pongezi si Wizara ya Madini wala si Doto Biteko bali ni Rais mwenyewe Dkt. John Pombe Magufuli na wadau wa madini kwa kukubali kufuata sheria”, alisema Waziri Biteko.

Wakati huohuo, Waziri Biteko amewataka Wachimbaji na wafanyabiashara wa Mkoa wa Geita kufanya shughuli ya Madini kwa kufuata sheria, kuepuka ukwepaji wa kodi na kutunza kumbukumbu ili kuepuka usumbufu usio wa lazima.

“Wilaya ya Chato ina jumla ya leseni za uchimbaji mdogo 276 ambapo ni yatatu baada ya Wilaya ya Geita yenye jumla ya leseni 630 na yapili ni Bukombe yenye jumla ya leseni 376 za uchimbaji mdogo wa Madini,” alisema Waziri Biteko.

Imeelezwa kuwa, mwaka 2017 kulifanyika marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010 ikiwa ni jitihada ya Serikali kudhibiti utoroshwaji wa Madini nchini ambapo, kifungu cha 27C (1 na 2) cha marekebisho ya Sheria ya Madini kinaelekeza uanzishwaji wa masoko ya Madini ambayo yana faida kubwa kwa wachimbaji, wafanyabiashara wa Madini na Serikali kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mbunge wa Chato ambaye pia ni Waziri wa Nishati, Dkt. Merdad Kalemani amempongeza Waziri Biteko kwa kazi nzuri anazozifanya na kueleza kuwa pamoja na maelekezo mazuri wanayo yapata kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, Wizara ya Madini imejipanga kuhakikisha inasimamia Sekta ya Madini kikamilifu na imeongeza pato la Nchi kwa kiwango kikubwa.

“Tulililia sana soko la Madini Chato, lakini leo tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kilio chetu kimepata majibu,” alisema Dkt. Kalemani.  

Nae, Rais wa Shirikisho la Wachimbaji Wadogo Nchini (FEMATA), John Bina amemuomba Waziri Biteko kuendelea kuwapa wachimbaji wadogo maeneo ya kuchimba na kaipongeza serikali kwa kugawa Transfoma saba kwa wachimbaji wadogo kila Mkoa.
=30=

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.