Na. Tito Mselem, CHATO
Tangu kuanzishwa kwa masoko ya Madini
nchini, Mkoa wa Geita umeongeza ukusanyaji wa mapato kwenye sekta ya Madini
kutoka chini ya shilingi bilioni 1 kwa mwaka mpaka kufikia zaidi ya shilingi bilioni
3.5 kwa mwaka.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Madini,
Doto Biteko alipokuwa akifungua soko kuu la Madini ya dhahabu Chato lililopo
Buseresere Mkoani Geita na kwamba, soko hilo limefikisha idadi ya masoko 29
nchini na masoko 8 yaliyofunguliwa Mkoani Geita ambalo kwa sasa lina ofisi 10
za madalali (Brokers) wanao nunua Madini hayo.
Aidha, Waziri Biteko amewataka maafisa
wa Serikali kutowasumbua wachimbaji na wafanyabiashara wa Madini pindi
wanapopeleka Madini yao sokoni na mchimbaji au mfanyabiashaya yoyote wa Madini
haruhusiwi kukaa na Madini nyumbani kwake bila ya kuwa na nyaraka kutoka
serikalini.
“Kipindi cha nyuma serikali ilikuwa
inatoa leseni kwa wafanyabiashara bila kujua wananunua wapi wala wanauza wapi
ila leo wanunuzi wanajua wakanunue wapi na wakauze wapi, haya ni mafanikio
makubwa sana kwenye sekta ya Madini na anae stahili pongezi si Wizara ya Madini
wala si Doto Biteko bali ni Rais mwenyewe Dkt. John Pombe Magufuli na wadau wa
madini kwa kukubali kufuata sheria”, alisema Waziri Biteko.
Wakati huohuo, Waziri Biteko amewataka
Wachimbaji na wafanyabiashara wa Mkoa wa Geita kufanya shughuli ya Madini kwa
kufuata sheria, kuepuka ukwepaji wa kodi na kutunza kumbukumbu ili kuepuka
usumbufu usio wa lazima.
“Wilaya ya Chato ina jumla ya leseni za
uchimbaji mdogo 276 ambapo ni yatatu baada ya Wilaya ya Geita yenye jumla ya
leseni 630 na yapili ni Bukombe yenye jumla ya leseni 376 za uchimbaji mdogo wa
Madini,” alisema Waziri Biteko.
Imeelezwa kuwa, mwaka 2017 kulifanyika marekebisho
ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010 ikiwa ni jitihada ya Serikali kudhibiti
utoroshwaji wa Madini nchini ambapo, kifungu cha 27C (1 na 2) cha marekebisho
ya Sheria ya Madini kinaelekeza uanzishwaji wa masoko ya Madini ambayo yana
faida kubwa kwa wachimbaji, wafanyabiashara wa Madini na Serikali kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mbunge wa Chato ambaye
pia ni Waziri wa Nishati, Dkt. Merdad Kalemani amempongeza Waziri Biteko kwa
kazi nzuri anazozifanya na kueleza kuwa pamoja na maelekezo mazuri wanayo
yapata kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe
Magufuli, Wizara ya Madini imejipanga kuhakikisha inasimamia Sekta ya Madini
kikamilifu na imeongeza pato la Nchi kwa kiwango kikubwa.
“Tulililia sana soko la Madini Chato,
lakini leo tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kilio chetu kimepata majibu,”
alisema Dkt. Kalemani.
Nae, Rais wa Shirikisho la Wachimbaji
Wadogo Nchini (FEMATA), John Bina amemuomba Waziri Biteko kuendelea kuwapa
wachimbaji wadogo maeneo ya kuchimba na kaipongeza serikali kwa kugawa
Transfoma saba kwa wachimbaji wadogo kila Mkoa.
=30=
Comments
Post a Comment