WAFANYABIASHARA WATAKIWA KUFUATA MATAKWA YA MIKATABA YA MASOKO DOODMA


Na. Jackline Kuwanda, DODOMA

Afisa Masoko wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, James Yuna amesema kuwa kila mtu anapotaka kuomba eneo la kufanyia biashara katika maeneo ya masoko kuna utaratibu unaotumika kwa lengo la kwenda sambamba na matarajio ya Halmashauri na wao kuheshimu shughuli za biashara zao ili ziweze kuwaletea tija.

Yuna aliyasema hayo jijini Dodoma wakati akizungumza na Mtandao wa Dodoma News ofisini kwake leo kuhusu taratibu za kupata eneo la kufanyia shughuli katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Afisa Masoko huyo amesema kuwa ipo mikataba mbalimbali ambayo mfanyabishara hulazimika kuingia na Halmashauri pindi anapohitaji kupata chumba kwa ajili ya kufanyia biashara kilichojengwa na Halmashauri.

“Tutampa chumba cha biashara, lakini tutampa mkataba wa upangaji ili aishi kwa uelewa wa mkataba huo na sisi tuwe tunafahamu anaishi mle kwa maelekezo gani ili kuepuka mambo ambayo hayatarajiwi kwenye maridhiano’’ alisema Yuna. Katika uwepo wa masoko katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, yapo makubaliano ambayo wamekuwa wakiyafanya na wafanyabiashara wakati wanahitaji nafasi ya kufanyia biashara katika maeneo ya Masoko, aliongeza.

“Kila mtu anapoomba eneo la biashara katika Halmashauri ya Jiji, tunautaratibu ambao huwa tunaoutumia. Tunamueleza kwanza atuandikie barua ili kuonesha nia yake kama anahitaji kupata eneo la biashara katika maeneo ya masoko ambapo anaiandika barua kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la dodoma ili kuomba nafasi, na sisi tunakuja kuangalia nafasi zilizopo na kuhakikisha tunampatia na kumtaka afanye biashara kwa mujibu wa mkataba’’ alisema Yuna.

Katika hatua nyingine amesema kuwa uwepo wa mkataba ni maridhiano ya pande zote mbili, huku akisema kuwa mikataba ina umuhimu mkubwa kwa sababu inafafanua haki ya kila mtu kutoka pande zote mbili.

“Mikataba inafafanua haki za kila mtu katika pande mbili kwa mfano mimi naweza nikawa nimekupangisha leo ukakuta nimemuweka mtu mwingine ana haki ya kwenda kushitaki na kudai haki yake’’ alisema Afisa huyo.  

Mbali na hilo amesema kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma halina masharti magumu wanachokifanya ni kuwaelekeza wafanyabishara licha ya kuwa na uwepo wa mikataba lakini kuna mambo mengi ambayo wamekusudia kuwanufaisha ikiwemo kuboresha masoko ambayo wafanyabiashara wataridhika nayo.

Hata hivyo, Yuna amesema ukishaingia kwenye mkataba wanatakiwa kufahamu  kuwa wako salama katika biashara zao na hakuna mtu yeyeto atakaye wasumbua wala yeyote kuingilia biashara zao.
=30=

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.