Mtumishi Wa Afya Akamatwa Na Polisi Kwa Tuhuma Za wizi Wa Dawa



Na. Editha Edward -TABORA

Mtumishi mmoja katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga Mkoani Tabora kitengo cha ugawaji dawa anayejulikana kwa jina la Francis Mlesa (33) anashikiliwa na Jeshi la Polisi Wilayani humo kwa tuhuma ya wizi wa a dawa zikiwemo za ARVs.

Akizungumza na Blog hii Ofisini kwake, Ofisa Tarafa ya Igunga mjini, Shadrack Kalekayo amesema tukio hilo lilitokea tarehe 24 Disemba, mwaka huu ambapo mtumishi huyo alishitukiwa na mlinzi aliyekuwa zamu majira ya saa Moja na nusu usiku baada ya kumuona amefunga maboksi mawili kwenye baiskeli.

Kalekayo amesema baada ya kukagua maboksi hayo ilibainika kuwa zilikuwemo dawa aina ya ARVs ila mtumishi huyo alifanikiwa kutoroka nazo baada ya mlinzi kuzidiwa na watu wanaopita getini hapo.

Mlinzi aliyekuwa zamu siku hiyo Rushina Paulo alithibitisha kumkamata mtumishi huyo na dawa hizo akidai kuwa zimeisha muda wake na akidai kuwa alikuwa anaenda kuziteketeza ila mlinzi huyo alipoziangalia aliona kuwa zilikuwa hazijaisha muda wake.

Amesema kuwa alitoa taarifa kwa uongozi wa Hospitali hiyo tarehe 26 Disemba, 2019 na alifikishwa mbele ya uongozi ambapo alikiri kuiba dawa hizo huku akisema alizichukuwa kwa ajili ya kuziteketeza moto. 

Kwa upande wa watumishi wa Idara ya Afya hospitalini hapo ambao hawajataka majina yao yajulikane wamesema mtumishi huyo amekuwa akiwauzia Wafanyabiashara wa Ng'ombe kwa ajili ya kunenepesha mifugo yao. 

Kwa upande wake kamanda wa TAKUKURU Wilayani hapo Fransis Zuakuu amethibitisha kuwepo kwa tukio hilo huku akisema alipigiwa simu na raia wema wakimjulisha kuwa kuna mtumishi ameiba dawa hospitalini na kutoroka nazo ambapo baada ya kumtafuta na kumkosa alimwagiza Mganga mkuu wa Wilaya hiyo Deus Ruha kumsaka ambapo Disemba 26 walimpata na tayari yupo mahabusu katika kituo cha Polisi wilayani hapo.

Aidha, Nzuakuu ametoa wito kwa watumishi wa idara zote kufanya kazi kwa uadilifu na kujiepusha na vitendo kama hivyo kwani Serikali haitafumbia macho mtumishi Yeyote atakayebainika na vitendo kama hivyo vya wizi wa dawa za Serikali. 

Hata hivyo Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Tabora ACP Barnabas Mwakalukwa alipoulizwa juu ya tukio hilo amethibitisha kushikiliwa kwa Francis Malesa huku akisema kwa sasa hawezi kuzungumzia suala lolote kwani bado wanaendelea kumhoji ili kubaini thamani ya dawa zilizoibwa.  
=30=

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.