Na. Mwandishi Wetu,
Faru Fausta ambaye alikuwa akiaminika
kuwa ndiye Faru Mzee zaidi Duniani amefariki akiwa na umri wa miaka 57 hapa
Nchini, Faru huyo ameishi maisha yake yote Katika hifadhi ya Ngorongoro mpaka
umauti ulipomkuta jana Disemba 27, 2019.
Mhifadhi mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya
Ngorongoro (NCA) Dkt. Fredy Manongi amesema Fausta ndiye alikuwa Faru mzee
zaidi Duniani.
"Tunahisi kifo chake ni cha
kawaida kutokana na umri wake kuwa mkubwa madaktari wapo njiani watatuelezea
hasa sababu ya kifo chake baada ya kufanya vipimo" ameeleza Dkt. Manongi
Aidha, Faru huyo jike alikuwa chini ya
uangalizi maalumu kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita baada ya afya yake
kudhoofika na kuanza kushambuliwa na wanyama wakali mwituni.
"Wanyama wakali hususani Fisi
walianza kumshambulia na akapata vidonda vikubwa sana lakini ilipofika mwaka
2016 ilibidi tumtoe porini na kumuweka kwenye uangalizi maalumu vidonda vyake
vilipona lakini afya yake bado ilikuwa dhoofu hatukuweza kumrejesha
porini" amesema Dkt. Manongi.
Faru Fausta licha ya umri wake kuwa
mkubwa hakuwahi kuzaa na hiyo inaelezwa huenda ikawa ni moja ya sababu ya
kuishi kwake kwa muda mrefu.
Hata hivyo Faru wanakadiriwa kuweza
kufikisha umri wa miaka 37 hadi 43 wakiwa porini na huweza kufikisha hadi miaka
50 wakifugwa katika maeneo maalumu, pia Faru mweusi mwingine wa mwituni ambaye
alifahamika kwa umri wake mkubwa ni Solio jike lililokuwa likiishi Kenya na
kufariki likiwa na miaka 42 mwaka 2016.
=30=
Comments
Post a Comment