DKT. BASHIRU: AWAOMBA WANANCHI KUPUUZA SERA NA KAULI ZINAZOHIMIZA UVIVU ZA BAADHI YA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA NCHINI
Na. Said Said Nguya,
BUKOBA
Katibu Mkuu wa
Chama Cha Mapinduzi, Dkt. Bashiru Ally, amewaomba wananchi kupuuza sera na
kauli zinazotolewa na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nchini zikitaka
wananchi wale bata (wafanye starehe) badala ya kufanya kazi jambo ambalo
likiachwa bila kukemewa litafanya kuwa na taifa legelege la kupenda starehe
badala ya kazi.
Dkt. Bashiru
amesema kuwa, katika nchi ambayo wananchi wanapambana kujikomboa kiuchumi, hasa
katika nchi zetu za Afrika ambazo bado tupo nyuma kimaendeleo ya mtu mmoja
mmoja na taifa kwa ujumla, kutokea kiongozi mmoja kuwaambia watu wafanye kazi
kwa starehe ni usaliti mkubwa wa mapambano ya kiuchumi ambayo kama taifa
tunayahimiza.
Katibu Mkuu
ameyasema hayo alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa ofisi ya CCM
Kata ya Bwanjai wilayani Misenyi tarehe 28 Desemba, 2019 na kuzungumza na
wanachama na wananchi waliojitokeza katika ukaguzi huo.
“Nchi hii ambayo
tunaongoza mapambano ya kujikomboa kiuchumi, inamuhitaji kila mtu kwa nafasi
yake kuhimiza kufanya kazi kwa bidii, na huku CCM kuna kauli mbalimbali za
kuhimiza kazi zikiwemo, Hapa Kazi tu, Kazi na Maendeleo, Uhuru na Kazi na Kazi
ni Utu, ila kuna baadhi ya Vyama wao wanahubiri kazi na starehe, na huo ndio
utofauti wa Chama kiongozi na Vyama vya uchaguzi.’’ Dkt. Bashiru ameeleza.
Ameongeza kwa
kusisitiza kuwa, “Unaposema kazi na bata, maana yake ni kudharirisha wanawake
na mama zetu ambao wakati wote wamekuwa wakifanya kazi kusomesha watoto wao,
wakifanya kazi kulisha familia zao, na sote hapa ni matokeo ya juhudi kubwa za
mama zetu, ambao kuwambia wale bata, ni sawa na kuwataka washinde kwenye
starehe huku watoto wakidharirika kwa kutokwenda shule, hizi ni kauli za
kipumbavu za Vyama vya uchaguzi, ambazo hatuna budi kuzidharau na
kuzipuuza."
Aidha ameongeza
kuwa, Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuwa chama cha kutetea haki za wanyonge
na kitaendelea kusisitiza sekta zote za serikali zikiwemo afya, elimu,
miundombimu na maji kutoa huduma kwa wananchi bila usumbufu wala ubaguzi
na kuthamini utu wa watu wote.
Mkutano huo
umehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali wakiongozwa na
Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kagera mama Costancia Buhiye na Mkuu wa wilaya ya
Misenyi Kanal Mstaafu Denis Mwila.
Ikumbukwe kuwa,
Dkt. Bashiru yupo nyumbani kwake Bukoba mkoani Kagera kwa mapumnziko ya siku
kumi, na anatarajiwa kumaliza mapumziko hayo mapema mwezi Januari, 2020.
Comments
Post a Comment