*KURUGENZI YA UKAGUZI WA MIGODI NA MAZINGIRA YAANDAA MWONGOZO WA UKAGUZI WA MIGODI*




Leo tarehe 27 Novemba, 2019 Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira imeanza maandalizi ya mwongozo utakaotumika kwenye ukaguzi wa migodi nchini.

Akizungumza katika kikao cha maandalizi  cha siku nne kinachoendelea jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Dkt. Abdulrahman Mwanga amesema lengo la mwongozo huo ni pamoja na kuwa takwa la Sheria na kupata taarifa sahihi za kaguzi mbalimbali kwenye migodi.
 
Kikao kikiendelea
Akizungumzia  namna shughuli zinavyofanywa na Kurugenzi yake, Dkt. Mwanga ameeleza kuwa, Idara imekuwa ikifanya kaguzi mbalimbali kwenye migodi mbalimbali nchini lengo likiwa ni kuhakikisha shughuli za uchimbaji wa madini zinaendeshwa kwa kufuata Sheria za Madini na Mazingira pamoja na kanuni zake.

Ameongeza kuwa, kati ya maeneo yanayokaguliwa kwenye migodi ni pamoja na karakana, sehemu za kuchenjulia madini, mabwawa ya topesumu,  vyanzo vya maji n.k. ili kuhakikisha hayaleti madhara kwa wafanyakazi wa migodi pamoja na wananchi wanaoishi jirani na migodi husika.

Ameongeza kuwa mwongozo wa ukaguzi wa migodi utaboresha kwa kiasi kikubwa kwenye shughuli za ukaguzi wa migodi nchini.

Wakati huohuo akizungumza katika kikao kazi hicho, Mkurugenzi wa Huduma za Tume, William Mtinya ameipongeza Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kwa hatua kubwa kwenye uandaaji wa mwongozo husika kama utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Tume ya Madini.

Ameitaka Kurugenzi kushirikisha wadau wengine ikiwa ni pamoja na Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa na kuongeza kasi ya ukamilishwaji wake ili uanze kutumika mara moja.

Aidha, Mtinya ameitaka Kurugenzi kuhakikisha mwongozo husika  unajikita kwenye uwekaji wa mazingira mazuri ya biashara hivyo kuboresha ukusanyaji wa maduhuli.

Naye Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba mbali na kupongeza Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kwa maandalizi ya mwongozo husika, ameitaka kutilia mkazo kwenye eneo la afya kwenye migodi pamoja na uboreshaji wa kanzidata (database).

Aidha, wafanyakazi wa Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira wakizungumza kwa nyakati tofauti mbali na kuwapongeza Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba na Mkurugenzi wa Huduma za Tume, William Mtinya kwa kuwatembelea wamesema kuwa wanaamini mwongozo husika utawarahisishia zoezi la ukaguzi kwenye migodi mbalimbali nchini na kutoa taarifa sahihi.


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.